FAQ katika kifungu cha Biashara

1 Mifumo ya kiuchumi, taratibu na kanuni za msingi zinatakiwa ziweje kwa mujibu wa Uislamu?

Mfumo wa kiuchumi wa Kiislamu haukubali ubepari wenye dhuluma wala ujamaa wa kikatili na ndoto. Kila mfumo usio sahihi unaweza kuwa na baadhi ya vipengele sahihi. Uislamu haukatai vipengele sahihi vya mifumo inayoikataa. Kama vile, mambo yanayokubaliwa na ubepari kama biashara binafsi, mali binafsi, biashara, sanaa na uchumi wa soko huria unaotegemea murabaha/kutengeneza faida kunaweza kuwepo na hilo lipo katika mfumo wa uchumi wa Kiislamu madam hazitofautiani na mwelekeo na maadili ya Uislamu. Kwa upande mwingine, mapambano dhidi ya faida haramu, dai la kukomesha mwanya baina ya matajri na masikini, mtazamo jumla dhidi ya riba katika uchumi, unaoonekana kuwa mbele zaidi katika ujamaa unaweza kukubaliwa na Uislamu kuwa ni miongoni mwa nukta sahihi.

Vipengele vinavyotokana na hadaa na kuhadaiwa na kuleta faida za haramu kama matumizi ya riba yameondoshwa katika Mfumo wa uchumi wa Kiislamu.

Mfumo wa uchumi wa Kiislamu unathaminishwa juu ya misingi ya kanuni kadhaa lakini masuala ya kiuchumi yatayotumika yameachiwa mazingira ya wakati na mahali madam mfumo huo haujakiukwa.

Kimsingi, Uislamu unaheshimu haki ya mali binafsi na uhuru wa mtu. Mmiliki ana haki ya kutumia mali yake atakavyo katika mfumo halali isipokuwa akiwa ni mtoto mdogo au hana akili timamu. Kama hana sifa za kutosha za kutumia mali yake, haki hiyo inaondolewa kutoka kwa mtu huyo. Ufujaji na israfu ni sababu muhimu ya kuondoshwa haki hiyo. Kanuni hii pia ipo katika mifumo na taratibu za kiraia za sasa.

Hata hivyo, Uislamu unazingatia israfu na ubakhili kuwa ni miongoni mwa vitendo visivyo vya kimaadili na kujaribu kuwaepusha watu na hayo kwa kuwaaibisha. Kwa kuwa Uislamu una yanayohusika na ahera, humzingatia mtu kidini kuwa anawajibika ingawa vitendo hivyo havimo katika sheria rasmi. Hii inawalinda Waislamu wasifanye ubadhirifu na kuwapeleka kwenye njia ya kiuchumi na ya wastani.

Tunakushauri usome makala yafuatayo yanayoitwa QURAN NA UCHUMI ya Prof. Dr. Osman Eskicioğlu:

Katika makala hii, tunayoiona inafaa kuiita Quran na Uchumi, tutajaribu kueleza kwanza Uislamu halafu uchumi baada ya hapo, kisha tutajaribu kutafuta na kueleza muunganiko baina ya hivyo viwili. 

Ninapaswa haraka sana niseme kuwa Quran inamhutubia mtu lakini ni kitabu kitukufu kinachomtaja Allah, malaika, mitume, ahera, mwanadamu, wanyama,  mimea na viumbe visivyo hai na kinachoueleza ulimwengu. Maana yake, Quran inataja kila kinachoweza kutambuliwa na hisia na pia viumbe wenye hisia za ziada. Kwa hivyo, ninadhani ni kupoteza muda kuuliza kuwa uchumi upo katika Quran au hapana.  

Ama kuhusu uchumi, kuna mamia ya tafsiri juu ya uchumi katika rasilimali za nyumbani na za kigeni lakini tunataka kufafanua uchumi kwa kifupi kuwa ni “sayansi ya kufanya kazi na kuishi” au “mfumo wa kufanya kazi na kuishi”. Uchumi unazingatiwa kuwa ni tawi la sayansi linalojitegemea katika ustaarabu wa leo lakini, kwa maoni yetu, sheria na kanuni zake bado hazijakamilishwa; tunadai kuwa ni uwanja wenye dosari na makosa kadhaa. Tunadhani kuwa ustaarabu wa kipindi cha Mwamko-Sanaa (katika karne ya 14, 15 na 16 huko Ulaya), kilifanikiwa sana katika mambo mengi lakini hakikufanikiwa kibinadamu na sayansi ya mwanadamu. Kama tutatoa mfano wa uchumi hapa, tunaweza kusema kuwa hakuna kodi iliyotumika Uturuki au ughaibuni iliyo ya kisayansi, kimantiki, inayofaa, ya haki na kibinadamu. 

Kabla ya kuanza kushughulikia hilo, tutakuwa na baadhi ya dhana ili mtazamo wetu ufahamike vyema na ulimwengu wa kiuchumi tunaoufahamu utabadilika kwa njia inayofaa katika mhimili wake. Katika mtizamo huu, dunia na ulimwengu vina mpangilio wa kiasili wa Allah. Inaonekana kana kwamba mwanadamu anatenda kama mwajiriwa katika kiwanda hiki cha ulimwengu, ambacho mwenyewe ni Allah na ambacho kina sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa na Allah. Anachopaswa kukifanya mwajiriwa huyu ni kutafuta, kufahamu jinsi kiwanda kinavyofanya kazi, na afanye kazi na kuzalisha kulingana na masharti ya kiwanda. Njia na uwanja wa kujifundisha wa mwanadamu ndio vyanzo vya dini na sayansi. Sayansi ni sheria na kanuni zinazoziambia hisia zetu na za vitu na mambo yanaweza kuingia katika maabara. Dini ni sheria na kanuni zinazouambia moyo wetu na vitendo na amali zetu zinazotegemea kukubali kwetu. Kwa hivyo, mwanadamu ni kiumbe anayeishi katika hatua inayopita nukta ambapo dini na sayansi vinakingamana. Vitendo vya hiari na visivyo vya hiari vipo ndani ya umbo la mwanadamu. Mwanadamu huhisi njaa, hutokwa jasho, huchoka na hujisikia baridi; Yaani, vitendo visivyo vya hiari humtokea mwanadamu. Havihusiani na dini; si vya dhambi wala malipo kwa upande wa dini. Hata hivyo, kula, kunywa, kuvaa, kufanya kazi na kuzalisha ni vitendo vinavyofanyika kwa hiari; hivyo, vimejumuishwa katika mawanda ya dini na vinatathminiwa kwa malipo au madhambi, sahihi au si sahihi na kufaa kwa matumizi au kudhuru. Ufafanuzi mwingine wa dini unategemea utashi; kwa hivyo, vitendo na amali zote zilizofanywa kwa hiari zinahusiana na dini; kimsingi, hivyo ni namna ya dini. Mwanadamu atahesabiwa kwa amali zake, vitendo, na mwenendo wake, huko ahera. Amali hizi zinaweza kuwa, sahihi au batili, zenye manufaa au madhara na madhambi au malipo. Hivyo, mwanadamu anaweza kujifundisha kipengele cha uchumi kinachohusiana na mambo yaliyo katika sayansi na kipengele chake kinachohusiana na mtu mmoja mmoja na jamii kutokana na dini; kisha, anaviunganisha na kuanzisha mfumo wake wa utendaji kazi na kuishi. Kanuni za dini na sayansi zilizowekwa na Allah; anachopaswa mwanadamu kukifanya ni kuzitafuta na kuzitumia.

Kwa hivyo, mwanadamu, kama ni mtu mmoja na kama ni jumuia, hana haki, uwezo au mamlaka ya kuingilia katika mfumo uliowekwa usio na mantiki kwa namna yoyote ile. Matakwa ya mwanadamu hayawezi kuwa dini au sayansi kwa sababu maisha ya manadamu ni sehemu ya ulimwengu na uchumi ni sehemu ya maisha ya mwanadamu. Ulimwengu ni mchanganyo wa sheria na kanuni. Zimeunganika kwa namna hiyo. Hata jua limekuwa katika mwelekeo wa mwanadamu (limepangiwa kazi ya kumzalishia mwanadamu bure, bila ya malipo yoyote). Mwili wa mwanadamu uko katika usawa; halikadhalika, kuna usawa wa kiasili wa kiungu katika maisha ya mwanadamu. Kwa bahati mbaya, ustaarabu wa leo umejaribu kuunda matabaka na vyama bandia ili nyanja katika maisha ya mwanadamu zitadumishwa na mizani itawekwa lakini tunaweza kusema kuwa imeleta madhara badala ya manufaa katika uchumi. Kwa hivyo, kwa rai yetu, vigezo, ufafanuzi na uchambuzi wetu hususani katika sayansi ya jamii inapaswa ipangwe upya; kitabu cha ulimwengu kinapaswa kisomwe tena na alfabeti zake zinapaswa ziandikwe upya.   

Kuna uzalishaji, matumizi, ushirikiano na kupeana hisa katika mwili wa binadamu kama ulivyo ulimwengu na maisha ya kiuchumi. Mifumo ya upumuaji, umeng’enyaji chakula, mzunguko na utoaji uchafu huchukua nafasi katika uzalishaji na utumiaji. Kama vile, damu, ambayo ni kitu, hugawanya mafungu katika namna ambayo hakuna haja ya kupigana, uadui baina ya matabaka, migomo au kufungiana nje; hivyo, kila mmoja anapata mahitaji yake katika namna bora kabisa. Waislamu watasimamisha mfumo wa aina hiyo wa kiuchumi, kama Allah ataruhusu, katika nuru ya sayansi na dini na chini ya nuru ya Quran na Sunnah kama jinsi ulivyo mwili wa mwanadamu.

Yanaelezwa yafuatayo katika Quran: Mwenyezi Mungu ameihalalisha biashara na ameiharimisha riba. (al-Baqara 2/ 275) Hivyo, uchumi wa Kiislamu umeelezwa kuwa unatofautiana na nyengine. Katika aya nyingine, yanaelezwa yafuatayo: Enyi mlio amini! Msiliane mali yenu kwa dhulma, isipo kuwa iwe biashara kwa kuridhiana wenyewe.(an-Nisa 4/ 29); kwa aya hii, uchumi wa soko huria umeoneshwa kwa sababu ya sharti la kuridhiana ni lazima katika biashara. “Kuridhiana” ni ridhaa inayoundwa moyoni kama Tabari anavyoeleza. (Ikhtilaf al-Fuqaha, uk. 146) Hili linawezekana tu katika mfumo ambao usambazaji na mahitaji hutokea kwa kujianzisha vyenyewe, uzalishaji na matumizi haviingilii na katika uchumi huria ambamo soko halilazimishwi, na bei ya chini, ukomo wa bei na bei zenye kuwekwa rasmi hazipangwi na serikali. Hata hivyo, ninaposema uchumi wa soko huria, ninapenda kusema hapa kuwa uchumi wa Kiislamu ni mfumo wa kipekee (sui generis) ukiwa pamoja na nyanja na tabaka zake zote.

Katika Uislamu, umiliki ni lazima katika uzalishaji kwa sababu ifuatayo inayoelezwa katika Quran: Na ya kwamba hatapata mtu ila aliyo yafanya mwenyewe? (an-Najm 53/ 39). Kwa hivyo, Kila mmoja atamiliki anachozalisha na kuuza kwa bei ya soko bila ya ulanguzi. Mwanadamu anamiliki kazi yake, pia; kwa hivyo, vyama vya kibiashara vinavyouza kazi za wafanyakazi havipo katika Mfumo wa Kiislamu. Hata hivyo, kuna nukta muhimu hapa. Wazalishaji wanamiliki bidhaa wanazozalisha lakini utumiaji ni wa jumuia ambamo bidhaa huzalishwa. Maana yake, kila mmoja ana haki ya bidhaa hizo wawe wanafanya kazi katika uzalishaji huo au hapana. Kwa hivyo, kila mmoja ana haki ya kuishi katika jamii ya Kiislamu. Mtume (s.a.w) ameeleza ukweli huu katika hadithi mbili zinazoonekana kama zinakinzana. Katika kueleza haki kuwa dola itachukua kisheria na kwa kutumia nguvu, Mtume (s.a.w) amesema, "Hakuna haki zaidi ya zakah katika bidhaa." (Ibn Majah Zakah, 3) Kwa upande mwingine, kuwa kukusudia sadaqah, ambayo mtu anatakiwa atoe kama haki ya kidini, kimaadili na ufahamu, amesema, "Kuna haki nyingine zaidi ya zakah katika bidhaa." (Tirmidhi, Zakah, 27, No: 659; Darimi, Zakah, 13) Ahmad Naim amekusanya maana ya hadithi hizo mbili kama ifuatavyo: Masimulizi ya Tirmidhi yanaeleza kuwa kuna haki nyingine inakusudia sadaqah (yaani, namna zote za sadaka na mali wanayopewa masikini kwa ajili ya Allah); na masimulizi ya Ibn Majah yanaeleza kuwa hakuna haki yanakusudia zakah (yaani, kodi inayokusanywa na dola ya Kislamu). (Ahmad Naim, Tajrid Sarih, I, 314).

Muhammad Hamidullah anasema kuwa zakah ni kodi inayokusanywa na dola ya Kiislamu kwa maneno yafuatayo: “Katika utamaduni wa Kiislamu, neno zakah hutumika kwa maana ya kodi inayochukua dola kila mwaka.” (Modern İktisat ve İslam, İstanbul–1963, uk. 17). Kama nilivyotaja katika utafiti unaoitwa “İslam ve Çağdaş Vergi Anlayışının Eleştirisi” (Uislam na Ukosoaji wa Ufahamu wa Kisasa wa Kodi) uliochapishwa katika mtandao wa www.enfal.de, mfungamano muhimu zaidi baina ya raia na dola ni kodi. Katika zama zetu, ni mtindo wa kisasa kusimamia dola kama watoto wanaocheza katika familia kadhaa; hivyo, kodi imebadilika na kuwa mwanasesere mikononi mwa serikali nyingi. Ninapaswa nikiri kuwa sikuweza kupata katika vitabu vya uchumi ufafanuzi unaostahiki wa kodi na sentensi za kweli na zinazofaa kueleza kwa nini kodi hukusanywa kwa sababu ustaarabu huu wa kipindi cha Mwamko-Sanaa (katika karne ya 14, 15 na 16), haukuweza kujua vyema dola na kazi zake na kujua ama dola ni kampuni ya kibiashara au taasisi inayofanya kazi kwa ajili ya pesa na mshahara au chombo kinachowahudumia rai bure kama familia ya asili. Kwa kuzingatia hadithi ifuatayo ya Mtume, sisi, kama jamii yenye mfumo, huzingatia jumuia na dola kama mfumo wa asilia kama familia si kama mkataba wa kijamii: “Waumini ni kama mwili kwa maana ya kupendana, kuhurumiana na kulindana. Kiungo kimojawapo cha mwili kinapougua, viungo vingine huugua pia na kukosa usingizi.” (Riyadhu’s Salihin (Bukhari, Adab 27; Muislamu, Birr 66). Familia inawahudumia wanawe bila ya kutoza malipo; halikadhalika, dola inapaswa kuwahudumia raia wake bure, bila ya kutoza malipo. Kwa hivyo, dola inawahudumia raia wake si kwa sababu huwa inakusanya kodi kutoka kwao lakini ni kwa sababu ni mlinzi na ni dola. Kama dola zingekuwa taasisi za kibiashara au kampuni zilizofanya kazi kwa msingi wa fedha, je isingekuwa muhimu kuwepo usawa baina ya kodi na huduma? Hata hivyo, haiwezekani kwa namna yoyote ile. Katika ufahamu wa Kiislamu, dola ni mlinzi; inakusanya kodi kwa sababu inachangia uzalishaji na inatumia kodi inayokusanya kuhudumia jumuia. Jambo hilo la matumizi ya bajeti katika uchumi wa Kiislamu linaelezwa katika aya ya 60 sura at-Tawba kuwa ni makundi 8.

Katika uchumi wa Kiislamu, kodi huletwa na uzalishaji; na kodi huwekwa katika uzalishaji. Inaelezwa waziwazi katika vitabu vya sheria ya Kiislamu na fiqh. Inamaanisha kuwa dola inakusanya kodi kama ni sehemu ya fungu lake kwa sababu inachangia kwenye uzalishaji. Hata hivyo, kodi hukusanywa kutoka katika uzalishaji na matumizi chini ya jina la kodi kwa leo. Hivyo, katika chombo ambapo masharti ya kuieleza jamii huandaliwa, kuleta ufumbuzi wa namna mbili kutokana na mambo mawili yenye kupingana inafaa kisayansi na mantiki au bila mantiki. Si jambo linalofahamika. Hitilafu nyingi hutumika katika maelezo ya dola kwa jamii na wachumi hunyamaza kimya.   

Tunaposema, "Kila mfumo unafanya kazi katika muundo wake wenyewe", kinachotakiwa kifahamike kutokana na hilo ni: uchumi ni mtangamano katika uwanja wake wenyewe na ni muhimu kuweka utangamano baina ya nyanja zinazounda jumuia kama sheria, maadili na uchumi. Kwa hivyo, bidhaa zinazozalishwa na uchumi zinakuwa halali kidini na zinaruhusiwa na, zaidi ya hapo, ni za kimaadili. Ninataka kutaja swali muhimu sana hapa. Uchumi katika ufahamu wa ustaarabu wa kipindi Mwamko-Sanaa (katika karne ya 14, 15 na 16) au ubepari si wa kimaadili. Şükrü Baban anaeleza yafuatayo katika mfululizo wa vitabu vyake viitwavyo "İktisat Dersleri" (Masomo ya Uchumi): “Matukio ya rai za kiuchumi kutokana na mtazamo wa faida. Hata hivyo, kama itaangalia tukio hilo hilo kwa mtazamo wa haki, itakuwa ni sheria. Kama tutalitazama kwa mtazamo wa maadili, itakuwa ni "maadili". Kasumba ina manufaa kwa mraibu wa hashish. Ufahamu huu unalingana na kanuni ya - kila kitu inayokidhi haja katika uchumi ni ya manufaa. Hata hivyo, inaweza kuwa si ya kimaadili kweli.” (uk. 7). Hii si sahihi kiakili kwa sababu mifumo katika mwili wa binadamu haikinzani yenyewe; bali hufanya kazi kwa utangamano. Nyanja katika jumuia ni kama hivyo au zinatakiwa ziwe kama hivyo. Kama sayansi au dini inasema hapana kwa ambacho uchumi unasema ndiyo, kama dini au uchumi unasema hapana kwa kile ambacho sheria inasema hapana, inamaanisha kuna mashindano baina ya nyanja katika jumuia ya aina hiyo. Kwa kuhitimisha, hakutakuwa na uchumi wenye afya, sheria na dini katika jamii ya namna hiyo. Kiungo kimoja cha mwili kinapougua, mwili mzima unaugua. 

Kama maisha ya kiuchumi hayakubaliani na amri na makatazo ya dini, uchumi wa namna hiyo hautakuwa wa afya kwa mujibu wa Uislamu. Kama vile, vilevi haviwezi kuzalishwa na Waislamu katika uchumi wa Kiislamu kwa sababu tu watu wanapata kazi na kufanya biashara. Yafuatayo yanaelezwa katika Quran: Enyi mlio amini! Bila ya shaka ulevi, na kamari, na kuabudu masanamu, na kupiga ramli, ni uchafu katika kazi ya Shet'ani. Basi jiepusheni navyo, ili mpate kufanikiwa. Hakika Shet'ani anataka kutia kati yenu uadui na chuki kwa ulevi na kamari, na akuzuieni kumkumbuka Mwenyezi Mungu na kusali. Basi je, mmeacha? " (al Maida, 5/90–91) katika hadithi, Mtume (s.a.w) amesema kuwa mtu anayetengeneza, anawafanya wengine watengeneze, anayekunywa, anayebeba, anayewafanya wengine wabebe, anayeuza, anayechuma riziki kutokana nayo, anayenunua, anayehudumia na anayetumia mali iliyochumwa kutokana na vilevi wamelaaniwa na amewakemea. (Abu Dawud, “Ashriba”, 2; Tirmidhi, “Buyu‘”, 58; Ibn Majah, “Ashriba”, 6). Kama inavyoonekana katika aya na hadithi hapo juu, vilevi vimeharamishwa; basi, tunahitimisha kuwa haviwezi kuzalishwa na kutumiwa na Waislamu.

Kama tulivyoona waziwazi kutokana na uzoefu, utendaji wa uchumi wa leo unahusiana na pesa. Kwa hivyo, tunaweza kusema kuwa kila uchumi wa zama hizi umeegemea kwenye pesa. Hata hivyo, hili ni jambo lisilo sahihi na lina madhara kwa sababu noti zimeenea katika soko la leo. Hata hivyo, noti hizo zenyewe hazina thamani hata kidogo. Huwezi kukidhi mahitaji kwa karatasi. Zina thamani ndogo mno. Thamani ndogo isiyo halisi; thamani iliyokisiwa na ya kufikirika tu. Basi, kitu ambacho chenyewe hakina thamani kinaweza kuwa kipimo cha thamani kwa sababu tu kinaitwa pesa? Pesa ya aina hiyo inawezaje kiuhalisia kuwepo katika kupima thamani ya bidhaa? Hivyo, inaweza kuonekana wazi kuwa kila uchumi ulioegemea juu ya pesa una kasoro.

Katika Uchumi wa Kiislamu, pesa ipo. Katika Quran, maneno "dirham" na "dinar" yanatajwa kama nyongeza kwenye mali". Hebu mtumeni mmoja wenu na hizi pesa zenu ende mjini. (al-Kahf 18/ 19) Neno rasilimali ni jina linalotumika kwa fedha, iwe imefanywa sarafu ama laa. Sarafu ya dirham au pesa inaitwa riqa, al-wariq. Wafasiri wamesema yafuatayo: Walikuwa na sarafu zilizokuwa na picha ya mfalme wao, mfalme wa mji unaoitwa Tarsus kwa leo. (angalia Fakhruddin Razi)

Na wakamuuza kwa thamani duni, kwa akali ya pesa. Wala hawakuwa na haja naye.” (Yusuf 12/ 20). Raghib ameeleza neno "dirham" kuwa ni sarafu ya fedha ambayo watu waliitumia katika kununua na kuuza. (Kitu Mufradat) Kwa upande mwingine, neno "dinar", linalomaanisha sarafu ya dhahabu, pia limetajwa katika Quran. (A. Imran 3/ 75) Hasan Basri Çantay alitoa sentensi ifuatayo wakati akitafsiri aya ambayo neno hilo limetumika: “Kama unamwamini kwa sarafu ya dhahabu, hatairudisha.” (Kur'an-ı Hâkim ve Meali Kerim, I, 94). Hivyo, baada ya maneno sarafu ya dhahabu na sarafu ya fedha, metali za dhahabu na fedha pia zimetumika katika Quran; kodi hutozwa juu ya metali za dhahabu na fedha ima ziwe ni sarafu au mikuo/vinoo. Kasani, mwanazuoni mkubwa wa fiqh ya Uislamu, anaeleza yafuatayo katika kazi yake inayoitwa Badayi'(I, 16): 5 dirham pia hulipwa kama kodi (zakah) pindi dhahabu, ambayo ni pesa kamili, na fedha vinapokuwa na uzito wa dirham 200. Yafuatayo yanaelezwa katika aya: Na wanao kusanya dhahabu na fedha, wala hawazitumii katika Njia ya Mwenyezi Mungu, wabashirie khabari ya adhabu iliyo chungu…” (at-Tawba 9/ 34) Kwa kuhitimisha, wanazuoni wa fiqh wanaziita dhahabu na fedha kuwa ni pesa kamili kwa sababu neno pesa lilitumika katika Quran kwa ajili ya dhahabu na fedha; Elmalılı amesema yafuatayo katika kitabu chake: "Wajibu wa dhahabu na fedha na sababu ya kuumbwa kwa namna ya kuwanufaisha wanadamu ni kuwa hizo ni njia za kubadilishana bidhaa, kuwa zinarahisisha kununua na kuuza na kuwa hutumika katika mahitaji halisi ya watu." (Hak Dini Kur'an Dili, IV, 324). Kwa hivyo, tunaizingatia kuwa ina umuhimu sana katika maisha ya kiuchumi kama dhahabu na fedha zitatumika kama pesa katika mzunguko kama zilivyokuwa zikitumika siku za huko nyuma. Tunadhani migogoro inayoibuka katika maisha ya kiuchumi leo, hususani mgogoro wa mwisho ulioitwa mgogoro wa kidunia uliokuwa katika ajenda duniani kote, unaanzia katika sera ya pesa. Dhahabu na sarafu za fedha zina thamani zake zenyewe kwa kadiri ya thamani yao. Sarafu za fedha zinaweza kutumika kama pesa ya taifa na sarafu za dhahabu zinaweza kutumika kama pesa ya kimataifa au ya ulimwenguni kote; hivyo, michezo inayochezwa kwenye vipande vya karatasi itaisha. Noti hizi husababisha serikali zitoe pesa za mkopo, ambayo ni sera isiyo sahihi; kwa upande mwingine, huwasababishia baadhi ya watu kughushi utoaji wa pesa za kughushi.

Kwa kuongezea, katika mgao wa mapato wa mfumo wa kibepari ambao upo kinadharia na kivitendo kote duniani leo, pesa pia hukopeshwa. Hata hivyo, ukopeshaji huo wa kulipa polepole unaitwa riba haujadhihirika kwa sababu noti yenyewe haina thamani; haitaweza kukidhi mahitaji kama bidhaa. Pili, pesa haidhuriki kadri inavyotumika. Kukodi hulipwa kwa sababu kitu kinachotumika hudhurika au kuharibika. Mpaka mwanzoni mwa karne ya 16, pindi ufahamu wa kibepari ulipoanza kuibuka, riba haikukubalika kuwa halali chini ya dini yoyote, falsafa mbalimbali, watu na taasisi; ilikatazwa na kuonekana ni haram; hata hivyo, ilizingatiwa kuwa ni halali chini ya Jean Calvin, ambaye alikuwa mwanamageuzi wa Kifaransa na mwasisi wa Ukalvani (mafundisho ya Calvin: kwamba kila kitu kilikwishaamuliwa na Mungu, amri ya Mungu) ambaye aliishi baina ya 1509 na 1564, kwa mara ya kwanza duniani. Baada ya Calvin kuiona riba kuwa ni halali, kanuni za kiraia za Genoa, ambazo zilikuwa chimbuko la Makalvani, zilihalalisha riba. John Knox wa Scotland na Henry VIII wa Uingereza waliondoa kabisa ukatazaji wa riba.

Miaka 50 baada ya Calvin, Claudius Salmosius, kiongozi mmojawapo wa Ukalvani, aliifanya riba kuwa huru na halali kikamilifu. 

Wachumi wa kimagharibi waliojaribu kuifanya riba ionekane halali waliishindania sana. Anwar Iqbal Qureshi anaeleza katika tasnifu yake ya udaktari iliyoitwa “Uislamu na Nadharia ya Riba” kuwa wanatanguliza fikra ifuatayo, inayoonekana kuwa ya maana zaidi: pindi mtu anapomkopesha pesa mtu mwingine au benki kwa mwaka mmoja, huwa anampa haki yake ya kutumia kwa mwaka mmoja. Mtu huyo huwa anampa mtu mwingine haki yake ya kutumia pesa zake na yeye ananyimwa haki yake ya kuitumia. Riba ni malipo yanayotokana nayo. Maelezo haya yanaweza kuonekana ya maana na yanaingia akilini lakini pesa hazichakai au kuharibika zinapotumika na hazipotezi thamani yake; kwa hivyo, maelezo haya hayatoshelezi. Basi, tunaweza kusema hivi: Pesa ni chombo kisichoweza kuzalisha thamani yoyote isipokuwa kitendo fulani, hatari au mambo kama hayo huongezewa. Kama mtu anayeikopesha benki ataiweka kabatini kwake badala ya benki, je, pesa yake itaongezeka baada ya mwaka? Kuna tofauti gani kati ya kuweka pesa katika sefu lake na kuweka benki? Hakuna tofauti. Basi, kwa nini pesa ya kabatini iongezeke inapowekwa benki? Quran inaeleza kuwa mifumo ya riba inazidisha migogoro kama watu wenye kifafa walivyo na kifafa: Wale walao riba hawasimami ila kama anavyo simama aliye zugwa na Shet'ani kwa kumgusa. Hayo ni kwa kuwa wamesema: Biashara ni kama riba. (al-Baqara 2/ 275)

Kuna kitu kingine zaidi kuhusu pesa katika uchumi wa Kiislamu. Kama inavyojulikana, katika desturi ya Uislamu, utoaji na utengenezaji pesa za sarafu ni haki ya dola; gramu moja ya pesa (dhahabu na fedha), thamani ya pesa na kuhifadhi thamani yake kuko chini ya udhibiti na usimamizi wa dola. Hivyo, haki juu ya pesa ni za dola na bidhaa ni za taifa na watu. Maana yake, mtu anaweweza kusia mbegu, kupanda mmea, kuzalisha na kuuza bidhaa bila ya kuomba ruhusa kutoka katika mamlaka yoyote ndani ya urari wa usambazaji na uhitaji, na uzalishaji na utumiaji. Dola haiwajibiki na uzalishaji, upangaji bei, uuzaji na kufanya mipango ya bidhaa; halikadhalika, mtu mmoja mmoja na jumuia hawana wajibu kuhusu pesa; ni wajibu wa dola, kwa sababu yanaelezwa yafuatayo katika Quran: na mshike Sala, na toeni Zaka, na mkopesheni Mwenyezi Mungu mkopo mwema.(al-Muzzammil 73/ 20) katika aya hiyo, ibara "mkopesheni Mwenyezi Mungu " ni maneno ya kisitiari. Katika sheia ya Kiislamu, "haki (sheria) za Allah" zinamaanisha "sheria ya umma". Baadhi ya haki zainaitwa hivyo kwa sababu sio za mtu mmoja mmoja bali zinahusika katika matumizi ya umma. Zinaitwa haki (sheria) kwa sababu ya umuhimu zilio nao. (Ö. N. Bilmen, Hukuk-ı İslamiyye, I, 226) Yaani, tunaweza kuhitimisha kuwa katika mfumo wa kibenki, benki zisizo za riba ni lazima; kunaweza kusiwe na benki za watu binafsi; benki za dola tu zinaweza kuwepo. Kwa kuwa uchumi wa Kiislamu ni uchumi wa urari kwa namna fulani, mtu mmoja mmoja na jumuia, mtu mmoja mmoja na dola zitakuwa katika urari zenyewe kwa maana ya uwanja; kwa upande mwingine, bidhaa na pesa zitawiana; bidhaa ni za taifa na pesa ni za dola.  

Nabii Shuayb (Jethro) alikuwa Mtume wa watu wa Madyan na Ayka. (Qurtubi, XIII, 135) Watu wa Madyan waliabudu masanamu. Shuayb aliwaita kwenye kumpwekesha Allah. Wao mara kwa mara waliwaghilibu watu kupitia vipimo vyao, mizani na sarafu za thamani ya chini. (Tajrid, VII, 295–296). Shuayb aliwaambia watu wake, Enyi watu wangu! Muabuduni Mwenyezi Mungu. Nyinyi hamna Mungu ila Yeye, wala msipunguze vipimo na mizani. Mimi nakuoneni mmo katika hali njema, nami nakukhofieni adhabu ya Siku kubwa hiyo itakayo kuzungukeni. Na enyi watu wangu! Timizeni vipimo na mizani kwa uadilifu wala msiwakhini watu vitu vyao; wala msieneze uovu katika nchi mkafanya uharibifu.(Hud 11/ 84–85) Aya hizi zinaonesha jinsi Nabii Shuayb alivyowaonya watu watii haki wakati wa kununua na kuuza bidhaa na si kuwaghilibu watu wakati wa kupima, n.k. Pia aliwaamuru waziwazi kuhusu kutokupunguza thamani ya vitu (bidhaa na pesa) za watu, zinazofunika hususani mfumuko wa bei katika zama zetu. Aya zinazofanana na zilizo katika sura Hud pia zipo katika sura al-Araf na ash-Shuara. Unaweza kuzirejea na kulinganisha. (al-Araf 7/ 85–93; ash-Shuara 26/ 176–191)

Aya hizi zinapochunguzwa, zinafahamika kutoka katika ushauri aliotoa na vipimo alivyochukua Mtume Shuayb ambapo aliwatuma ili kurekebisha vyema uchumi uliodidimia. Jambo mojawapo muhimu zaidi alilofanya lilikuwa ni mapambano yake dhidi ya mfumuko wa bei. Kwa kuwa mfumuko wa bei ni chanzo cha aina zote za dhuluma na uovu na kwa kuwa waliosababisha mfumuko wa bei kwa kupunguza dhahabu na sarafu za fedha walisababisha dhuluma pamoja na mfumuko wa bei, Mtume Shuayb alikataza hilo. Kwa mujibu wa masimulizi ya Zayd b. Aslam, Watu wa Madyan walikata dhahabu na sarafu za fedha kama dhahabu na fedha; kisha, wakawapa watu kwa kuzihesabu lakini pindi walipozichukua sarafu hizo zilizokatwa kutoka kwa watu, walizipima. Walipochukua sarafu nzuri kutoka kwa watu, walizihesabu lakini walizipima zilizokatwa na kuwa na thamani ya chini wakati wa kuzipokea. Hili lilimaanisha kuwaghilibu watu. Mtazamo wao huu, maana yake, wakati mwingine kwa kuhesabu na wakati mwingine kupima sarafu, kulisababisha hasara katika bidhaa na dhuluma. Allah alipeleka ghadhabu kwa watu wa Madyan kwa sababu hawakuacha na Akawaadhibu. (Tabari Jami’ul Bayan, XII, 102; Ayni XII, 246; Tajrid, VII, 295–296). Maana yake, kama tutaitafsiri kwa hali ya sasa, tunaweza kusema kuwa watu wa Madyan waliangamizwa kwa sababu ya mfumuko wa bei.

Kwa mujibu wa masimulizi kutoka kwa Ibn Abbas, walikuwa wakorofi. Waliwadhulumu watu mara kwa mara. Pindi mgeni alipoenda katika nchi yao, walimzuia kabla ya kuingia katika mji wao na kuchukua sarafu zake, kwa kusema kuwa pesa zake zilikuwa za kughushi au zimekatwa na wao humlipa pesa pungufu. Hii ilikuwa ni dhuluma. Kwa hakika, walikatazwa kwa kupima kimakosa bali pia na makosa yote ya kifedha. (angalia Alusi, Ruh-ul Maani, VIII, 177)

Yafuatayo yanaelezwa katika tafsir ya Qurtubi: walikatazwa kukata sarafu lakini hawakutii makatazo hayo; kwa hivyo, wakaangamizwa. Walikuwa wakikata sarafu nzuri ili kupata manufaa yasiyo ya haki. Pindi waliposhughulikia sarafu nzuri, walizihesabu lakini waliposhughulikia zile zilizokatwa walizipima na kuwaghilibu watu. (Qurtubi, al-Jami li-Ahkam-il Qur'an, IX, s. 88). Hawakumtii Mtume wao, Shuayb na wakamdhihaki kwa kumwambia kwa ujeuri: Ewe Shua'ibu! Ni sala zako ndizo zinazo kuamrisha tuyaache waliyo kuwa wakiyaabudu baba zetu, au tuache kufanya tupendavyo katika mali zetu? (Hud 11/ 87). Hivyo, walisema kuwa wangetumia bidhaa zao kama walivyotaka; wangezikata, kuzitupa au kuziunguza. (Tabari, Jami’ul Bayan, XII, 102). Hata hivyo, ni muhimu kuwalipa watu kiasi kinachostahiki bila ya upungufu wowote bila ya kujali kama bidhaa zao zimepimwa uzito, ujazo au kipimo chochote. (Tabari, XII, 99; XIX, 108).

Mtume Shuayb alitumwa Madyan, ambapo aliishi, na pia Ayka, mji mwingine. Aliwahutubia watu wa Ayka kama ifuatavyo: Timizeni kipimo sawa sawa, wala msiwe katika wanao punja. Na pimeni kwa haki iliyo nyooka; Wala msiwapunje watu vitu vyao, wala msifanye jeuri kwa ufisadi. (ash-Shuara 26/ 181–183). Ni nini maana ya "kutokuwasababishia wengine hasara" ni msikate sarafu na kukiuka haki za watu kwa kuwaghilibu. (Alusi, Ruh-ul Maani, XIX, 118).     

Kama inavyoweza kuonekana, aya inapochunguzwa kwa makini, watu hawana haki ya kutumia bidhaa zao namna watakavyo. Kwa kusema, "Tunaacha kufanya tunachokipenda kwa kutumia mali", wanazungumza kwa dhihaka wanaposema "kwani swala zako ndizo zinazokuamrisha hivyo?" Wanajifanya kana kwamba wana haki ya kufanya chochote wakitakacho kwa bidhaa zao. Inafahamika kutokana na aya hiyo kuwa mwanadamu hawezi kufanya chochote atakacho katika bidhaa zake na kuzitendea atakavyo. Bidhaa zina sheria na kanuni zinazozishughulikia; yaani, zina haki. Muhuri wa asili uliopo juu ya kila kiumbe wa kiasili umepigwa kwa uwezo wa Allah. Viumbe wana muhuri wa Allah juu yao; hivyo sheria na kanuni za kiasili katika asili zao haziwezi kubadilishwa na wao wenyewe au watu. Maisha ya binadamu na maisha ya viumbe wote hai na wasio hai yamepangiliwa kwa utashi wa Allah. Kwa hivyo, Mawdudi anaeleza yafuatayo wakati akitafsiri aya hii: “Uhitaji wa kabila la Nabii Shuayb kutumia bidhaa zao kama walivyotaka unaonesha kuwa jambo jipya halikuongezwa katika nadharia ya kugawanya maisha katika sehemu mbili, ya kidini na ya kidunia.”(Tafhim, II, 418)

Elmalılı aliandika yafuatayo kuhusu jambo hilo: Walilizingatia hilokuwa jambo linalozuia uhuru au upumbavu kumwabudu tu Allah kwa kujiondoa katika kuwa watumwa wa miungu ya aina mbalimbali na kutii kanuni za sheria na maadili katika biashara na siasa. Nabii Shu'ayb hakuwaomba kuwa wasifanye watakavyo kwenye bidhaa zao. Alisema, "Wala msiwapunje watu vitu." Haikumaanisha kuzuia uhuru; kinyume chake, ilimaanisha kuweka na kuimarisha uhuru. Hakuna ambao wangekuwa na hakika ya haki zao na kufanya chochote walichokitaka katika bidhaa zao kama bidhaa za watu hazikuwa salama. Hata hivyo, walizitazama  bidhaa za watu wengine kama bidhaa zao wenyewe na wakawadhulumu kadri walivyoweza. Kamwe hawakujali haki; hawakuepuka mambo ya haramu. Waliyazingatia maonyo ya Nabii Shu'ayb kuwa ni kizuizi cha uhuru wao. Walijaribu kumdhihaki kwa njia ya kumfitini: "Kwani swala zako zinakuamrisha kuwa tuache kufanya tunavyopenda kwenye mali zetu? Ewe mchamungu! Wewe ni mwerevu sana!" Hivyo, kwa upande mmoja, waliabudu masanamu na kwa upande mwingine, walimfanyia Allah kiburi na waliitweza swala. Licha ya hayo, kufanya ulaghai, kutokuheshimu haki na kufanya kiburi chini ya jina la uhuru na biashara, na kuutukana utume ni katika maradhi ya enzi za Jahiliyya ambazo pia zimeena baina ya makafiri wa leo. Kwa hivyo, watu wa leo wanapaswa kusikiliza kwa umakini sana kisa cha Shuayb na mwisho wa watu wa Madyan. (Elmalılı, Hak Dini, IV, 561–562).

Majukumu kama ya kuhifadhi dini, akili, nafsi, kizazi na mali yalizingatiwa ni katika vipengele visivyoepukika na maeneo muhimu ya maisha kwa rai za wanazuoni wengi tangu kwa Juwayni (419–478/ 1027–1098), mwalimu wa Ghazzali mpaka Ghazzali mwenyewe na Shatibi. Kuhifadhi mali, ambako ni mojawapo katika maeneo hayo matano, hakuhusu kukataza wizi tu. Kunahusu mkusanyiko wa sheria na kanuni zinazofunika eneo lote la kiuchumi na zinalinda mali kwa kutumia sheria za asili juu ya mali.

Kuna jambo linalovutia hapa, pia; kwa mujibu wa hili, eneo la kiuchumi linafunika sehemu 1/ 5 au 20% ya maeneo muhimu. Kiasi hicho hicho kipo katika swali kuhusu fungu la dola katika ngawira iliyotajwa katika Quran: Na jueni ya kwamba ngawira mnayo ipata, basi khums (sehemu moja katika tano) ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na Mtume, na jamaa, na mayatima, na masikini, na wasafiri…Na Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu.(al-Anfal, 8/ 41) Kwa kuzingatia ukweli huu, tunafahamu na kukubali kuwa eneo la kiuchumi lina eneo, muda, mahali na thamani ya 1/5, likiashiria kuwa dola ina mamlaka ya 1/5 katika uchumi. Tunaweza kusema kuwa katika uchumi wa Kiislamu, mali ya binafsi ina eneo la 80% na dola ina eno la 20%. Kwa hivyo, tunaweza kusema kuwa uchumi ulioshauriwa na Quran au uchumi wa Kiislamu ni uchumi wa soko huria.

Tunaposema uchumi wa soko huria hapa, kuna jambo tunalohitaji kueleza mara moja. Maneno hayo yana asili ya Kimagharibi na muhuri wa ustaarabu wa kipindi cha Mwamko-Sanaa (katika karne ya 14, 15 na 16 huko Ulaya). Hatuwezi kuufikia Mfumo wa Kiislamu kwa maneno ya Kimagharibi maneno na maelezo na rai na dhana na fikra zilizoletwa na watu wa Magahribi. Maana yake, kunaweza kuwa na baadhi ya vyenye kufanana kati ya uhuru wa Uchumi wa Kiislamu na uchumi wa soko huria, lakini tofauti zipo, pia. Kwa hakika, ufahamu wa uhuru wa Kimagharibi unamaanisha kumpa uhuru mtu kutoka katika eneo la chini ya amri ya dola. Kwa maneno hayo, tunaweza kusema kuwa watu na dola kila mara hupishana wao kwa wao kwa sababu ufahamu wa Kimagharibi hauwezi kuainisha vyema mahali pa mtu mmoja mmoja na dola. Hata hivyo, jambo kama hilo haliwezekani katika Uislamu. Mtu mmoja ni fardh ayn; jumuia (dola) ni fardh kifayah. Ubaguzi wa wanachama wa Wapablikani/Wanajamhuri na Wademokrati katika maisha ya kisiasa huko USA unaonesha waziwazi ubishani na kupingana huku, ambao ni dhahiri kuwa si sahihi. Kama tunafananisha dola na dari ya nyumba, sakafu itakuwa watu. Baadhi ya watu wanaoishi katika nyumba hii wanashikilia dari na kuitegemeza; wengine wanaitegemeza sakafu au msingi. Je, jambo kama hili linawezekana? Je, kunaweza kukawa na nyumba bila ya dari au bila ya msingi? Kwa hivyo, katika jumuia ya Kiislamu, mtu anaunga mkono vyote viwili, hali ya mtu mmoja mmoja na dola. Hali hii inafanana na mtu anayeishi katika familia. Kila mwanafamilia anatakiwa kutambua, kujali na kufikiria vyote viwili, nafsi yake na familia; wanatakiwa vyote viwili waviweke katika uwiano. Tunasema, kila tawi la sayansi, kila ustaarabu na mfumo una istilahi, maelezo na madaraja yaliyo wazi wazi kwao. Sisi, kama Waislamu, hatujaweza kuleta maneno na istilahi zetu wenyewe na kuanzisha jumuia yetu wenyewe; kwa hivyo, tunalazimika kutumia maneno na istilahi zilizoko sokoni kwa kusema kuna uchumi wa soko huria katika Uislamu. Hata hivyo, kama kuna haki au matumizi ya kuanzisha benki binafsi katika uchumi wa soko huria, na kama ni ulazima wa uhuru huu, tuna haja ya kusema kuwa hakuna uhuru wa namna hiyo katika uchumi wa Kiislamu na kuwa mabenki ni mali ya dola katika Uislamu.

Tunapo sema soko huria (serbest piyasa) kwa Kituruki, asili ya neno "piyasa" ni neno la Kiitaliani “piazza”. Neno hili linamaanisha mraba, kituo cha mauzo na soko. Asili ya neno "pazar" kwa Kituruki linatokana na Kiajemi "bazaar"; linamaanisha mahali pa manunuzi, mahali pawazi kwa ajili ya manunuzi. Kwa Kituruki maneno yote mawili hutumika kwa ajili ya “marché” kwa Kifaransa, “market” kwa Kiingereza na “soko” kwa Kiswahili. (H.Atıf Kuyucak, İktisat Dersleri, İst. Üni. İkt. Fak. Yayınları, 1960, uk. 197, tanbihi: 2).

Ibara ya soko huria ina fikra na ufahamu wa uchumi wa Kimagharibi kabisa. Inapaswa ifahamike na kukubalika hivyo. Kama tunasema lipo soko huria au halipo katika Uislamu kwa utambuzi wa wanachomaanisha wasomi wa uchumi, tutafanya kosa kwa sababu neno soko huria lililotumiwa na wasomi wa uchumi na wachumi wa Kiislamu hawamaanishi jambo hilo hilo.

Samuelson anatoa maoni kuhusu maneno hayo. Maneno yafuatayo ya Samuelson yanaweza kuzingatiwa kama ustaarabu wa Kimagharibi unaokiri udhaifu kuhusu sayansi za kijamii na hususani uchumi. Licha ya hayo, kwa rai yetu, ulimwengu wa Kimagharibi haukufanya sayansi ya uchumi kwa kukamilisha istilahi zake, ufafanuzi na uainishaji. Baada ya kusema kuwa tunapaswa tujilinde dhidi ya matumizi ya istilahi hususani katika sayansi za kijamii, Samuelson anaeleza kuwa hatutakiwi kutumia istilahi mbili kwa dhana hiyo hiyo moja na tuoneshe mambo mawili tofauti kwa neno moja. Kisha, anatoa mfano ufuatao ili kuweka wazi jambo hilo: Jones anamwambia Robinson, anayedai kuwa kinachosababisha mgogoro ni kuzidisha uwekaji akiba: "Umekosea; sababu halisi ni matumizi yasiyotosheleza." Schwartz, anayewasikia, anaingilia mazungumzo na kusema, "Nyote wawili mnaongea upuuzi; sababu hasa ni uwekezaji usiotosheleza." Kwa hakika, kama wataacha kubishana kwa kitambo na kuchanganua na kulinganisha maneno wanayotumia, wataona kuwa madai yote matatu yanayoonekana kutofautiana kwa hakika ni kitu kilekile kimoja na kwamba tofauti inaanzia katika utata wa istilahi. (Paul A. Samuelson, Economics, uk. 10) 

Istilahi za uchumi wa kisasa na istilahi za uchumi wa Kiislamu zinatofautiana. Mfano mzuri ni neno "mal" (bidhaa, mali). Katika sheria ya Kiislamu au uchumi, kitu kinatakiwa kiwe halali kidini na kiwe na uwezo wa kukidhi mahitaji ili kizingatiwe kuwa ni "mal". Kutokana na hayo, pombe na nyama ya nguruwe, ambavyo vimefanywa haram, havizingatiwi kuwa ni "mal" kwa Muislamu; halikadhalika, nafaka chache hazizingatiwi kuwa ni "mal" kwa sababu haziwezi kukidhi mahitaji. (Angalia Ibn Abidin, IV, 3; M. Mutahhari, İslami İktisadın Felsefesi, trans: Kenan çamurcu, İst. 1995, Uk. 33; Majalla, kipengee 126 na 127)

Neno fikra za mabadiliko ni jina la tapo katika historia ya uchumi. Tapo hilo linaitwa tapo la wanamabadiliko pia ni tapo la idara ya sanaa ya juu sana. Wafuasi wa tapo hili hawakubali uingiliaji wa dola katika uchumi; wanashikilia rai kuwa mtu mmoja mmoja ana uhuru. (İbrahim Fadıl, İktisat, İst. 1928, uk. 43–45). Wanaendeleza fikra ya sheria ya uasili-ya kiungu ya Wafuasi wa Physiocracy, waliojitokeza kama mjibizo kwa Wafanyabiashara, na akadai kuwa uchumi utakuwa unasimamiwa na mkono usioonekana pamoja na ukombozi wa mtu mmoja mmoja. Ibara “Laissez faire, Laissez passer” (hebu tufanye na hebu tufaulu) iliyobuniwa na Gournay, ambaye ni mfuasi wa Physiocracy, ikawa mbiu ya tapo la mabadiliko. (Feridun Ergin, Ak İktisat Ans. S. 355) Kiasili, mwanadamu amefikia fikra hii ya uana-mabadiliko katika uchumi baada ya baadhi ya hatua za kiuchumi, baada ya kukumbana na madhara ya makatazo, vizuizi na uingiliaji kati.

Uanamageuzi pia unaitwa ubinafsi kwa sababu unaamini kuwa utu unaweza kupanda kiyakinifu na kiroho kwa juhudi za mtu mmoja mmoja. (İbrahim Fadıl, İktisat, uk. 45) Kwa hakika, uchumi wa kisasa umekuwa kama uchumi wa jumuia au kwa maneno mengine, kama uchumi wa dola. Makabaila walipoanza kuporomoka taratibu baada ya karne ya 15 na dola kubwa zilipoanza kuanzishwa, uchumi ulianza kuweka mahusiano ya siasa na dola. Kwa hakika, mchumi wa Kifaransa aliyeitwa Antoine de Monchretien aliunganisha maneno siasa na uchumi kwa mara ya kwanza na kuchapisha kitabu kilichoitwa “Economie Politique” katika mwaka 1615 (Feridun Ergin, İktisat, uk. 1; Ak İktisat Ans. uk. 685; İbrahim Fadıl, İktisat, uk. 40) Magharibi ilikuwa ya kikonomisti hapo awali ambapo Adam Smith, anayezingatiwa kuwa ameasisi nadharia ya ubinafsi na nadharia ya mabadiliko, alikiita kitabu chake mashuhuri “Mali ya Mataifa”. (angalia Adam Smith, Milletlerin Zenginliği, trans: Haldun Derin, Milli Eğitim Basımevi, İst. 1948

Baada ya kutoa maelezo kuhusu tapo linaloamini Physiocracy (nadharia ya kiuchumi iliyoletwa na wachumi wa kifaransa katika karne ya 18 kuwa utajiri wa mataifa umepatikana kutokana tu na uendelezaji kilimo au ardhi), tumetaja masharti na dhana zilizoandaa na zilizoutathmini katika istilahi za sheria ya Kiislamu katika kitabu chetu kiitwacho “İslam Hukuku Açısından Serbest Piyasa Ekonomisi (Uchumi wa soko huria kutokana na Mtazamo wa Sheria ya Kiislamu)”. Wenye nadharia hiyo ya Physiocracy ndio wachumi wa mwanzo waliosema kuwa kulikuwa na sheria ya kimaumbile ya kiungu ulimwenguni na kwamba uchumi ulifanya kazi kwa kutegemea sheria za utaratibu huo wa kimaumbile. Kwa hivyo, inawezekana kusema kuwa watu wa nadharia ya-Physiocracy wana fikra zinazolingana na Uislamu "kwa sababu Uislamu ni dini ya kimaumbile kwa mwanadamu na kwamba imekusanya sheria za kimaumbile. Maumbile ni sheria ya uumbaji wa Allah na Uislamu ni sheria Yake ya kiutendaji. Kwa hivyo, hakuna amri iliyo kinyume na sababu na maumbile katika Uislamu.” (Ahmet Hamdi Akseki, İslam uk. LXX (70))

Elmalılı anaeleza yafuatayo kuhusu jambo hilo: Kwa hakika, kwa kuwa Allah ni Mola Mlezi wa ulimwengu, sheria Zake zinafanya kazi ulimwenguni kote. Sheria wakati mwingine hutajwa kwa jambo linaloziweka na wakati mwingine baada ya mada zinazohusiana nazo. Kama vile, Sheria za Solon (Soloni ni neno la Kigiriki lenye maana ya mtoaji sheria) zimetajwa kwa jina la mtu aliyeziweka; sheria za mali isiyohamishika zimetajwa kwa jina la mada. Maumbile yako chini ya amri ya sheria-iliyowekwa na Allah; kwa hivyo, sheria hizo zinaitwa "Sheria za Kimaumbile". Hata hivyo, inafaa zaidi kuziita sheria za Allah na mfumo wa kiungu kwa kuwa Allah ameziweka zote hizo… Kwa hivyo, mwanadamu anachohitajika kukifanya si kuweka sheria katika sayansi na dini bali kutafuta na kupata sheria za Allah na kuzidhihirisha. Si sahihi kusema kuwa Archimedes aliweka sheria ya elimumituamo ya maji (hydrostatics), Newton ameweka sheria ya mvutano na Aristotle ameweka sheria ya kutokuwepo ukinzani; si sahihi kusema Abu Hanifa ameweka sheria za ulinganishi na fiqh, pia. Kama sheria hizo wangeziweka wao, zisingekuwa sahihi. Hao wamepatia kwa sababu hizo ni sheria za Allah zilizogunduliwa. Kwa hivyo, wanasayansi na wanazuoni sio wanaobuni bali huvumbua na kudhihirisha. (Elmalılı, Hak Dini, I, 126)   

Katika uchumi wa Kiislamu hakuna ukinzani baina ya kanuni za uzalishaji, utumiaji, kubadilishana, mzunguko na kodi; hakuna hali ya kutotangamana baina ya uchumi na dini na baina ya maadili na sheria, pia. Kwa upande mwingine, hakuna ukinzani au kutokutangamana bali kutangamana baina ya mtindo wa maisha ya nasaha za Uislamu kwa mwanadamu na jumuia, na dunia na ulimwengu. Hata hivyo, maneno na istilahi za mifumo mingine haziwezi kueleza ufahamu wa Kiislamu. Kama vile, pindi sentensi "kuna uchumi wa soko huria katika Uislamu" inapotamkwa, haimaanishi uchumi wa soko huria wa wanamabadiliko na ufahamu wa Kimagharibi. Tunauzingatia ufahamu wa wanamabadiliko wa Magharibi kuwa wa aina yake. Imeonekana waziwazi hususani katika sanaa yao, ushairi na fasihi. Hata hivyo, hakuna hali ya upekee katika Uislamu na maisha ya kiuchumi yaliyoshauriwa nayo kwa sababu yanaelezwa yafuatayo katika aya: “Ati anadhani binaadamu kuwa ataachwa bure? (al-Qiyama 75/ 36) Maisha ya kawaida na ufanyaji kazi wa mazingira ya kiafya yanategemea sheria na kanuni; halikadhalika, hata maisha yasiyo ya kawaida na utendaji mbaya wa jumuia hutegemea sheria na kanuni. Maana yake, hakuna kutokufuata kanuni katika ulimwengu wa viumbe; hata watu waovu na jumuia zenye uovu hutenda kwa kuzingatia kanuni. Allah ndiye aliyeziweka sheria na kanuni hizo juu ya maumbile, na maisha ya kijamii na  ya kiuchumi. Sisi tunatumia sheria na kanuni hizi zilizowekwa na Allah kupitia katika dini na sayansi juu ya mambo ya kiuchumi, maana yake, kwa namna anavyotaka Allah. Kwa hivyo, Uislamu hautazami tamko la nia linalotosheleza katika mambo ya kiuchumi kama katika mambo ya kijamii; kwa kuongezea, unaiweka kama sharti kwa pande mbili kuwa na ridhaa. Tunaita matukio ya mahusiano ya kijamii ya daktari-mgonjwa, mwalimu-mwanafunzi, dola-raia na mume-mke. Tunazingatia kuwa kutamka nia kunatosha kutumia haki hizo. Ibn Abidin anaeleza yafuatayo kuhusu jambo hilo: "mkataba wa ndoa, talaka na kumpa uhuru mtumwa ni halali kwa nguvu na bila ya ulazima wa ridhaa. Kama mtu atampa talaka mkewe kwa dhihaka, mkewe atazingatiwa kuwa ameachika kisheria lakini si kidini.” (Ibn Abidin, II, 421; cf: Kasani, V, 176). Miamala ya watu inayoegemea juu ya bidhaa, juhudi na pesa inaitwa mambo ya kiuchumi; baada ya kutamka nia, maana yake, kutoa na kupokea, ridhaa pia ni muhimu. Kwa hivyo, ni muhimu mtu kuridhia namna zote za miamala ya kiuchumi anayoileta kwa juhudi zake, ananunua na kuuza. Je, inawezekana kusema kuwa wafanyakazi swanaridhia makubaliano ya pamoja kama kundi yaliyosainiwa na viongozi wa muungano wa kibiashara kwa niaba yao (!) leo?
Kanuni zifuatayo ni muhimu ili soko huria lijitokeze wenyewe katika uchumi wa Kiislamu:  

1- Lazima kutokufuja mali ya watu kwa dhuluma na kutonunua, na vitu viuzwe kwa kutumia mkataba wa kubadilishana na makubaliano ya kibiashara unaozingatia ridhaa ya pande mbili. Tumeshaeleza aya inayohusu jambo hilo hapo juu. 

2- Kukataza riba na ulanguzi ni kanuni mojawapo iliyowekwa na Uislamu. Kama wanazuoni wa Kiislamu walivyosema, riba ni kitu cha ziada kisicho na ulinganifu. Bidhaa na pesa katika uchumi ni kama damu katika mwili wa binadamu; hivyo, ni lazima waendelee kuzungusha. Kwa hivyo, ulimbikizaji au kuweka mahali kama ziada itavimba kama saratani mwilini na kusababisha maradhi na mgogoro. Tumeshaandika aya inayohusu jambo hilo hapo juu.

Ulanguzi unamaanisha kuweka bidhaa ambazo watu wanazihitaji kwa kutarajia kupanda kwa bei zake. (Kamil Miras, Tajrid, VI, 448). Kuna hadithi kadhaa kuhusu jambo hilo. Kama vile, Muadh b. Jabal anasema: Nilimuuliza Mjumbe wa Allah kuhusu yaliyomo kwenye ulanguzi. Akasema, “Mtu hufurahi anaposikia kuwa bei iko chini na husikitika pindi bei zinapopanda. Ama kuhusu mlanguzi, huyo ni mtu mwovu; yeye husikitika kama Allah anashusha bei na hufurahi Anapozipandisha. (Haythami, Majmau’z Zawaid, IV, 101; Mansur Ali Nasif, at-Taj, Buyu, 2) Imesimuliwa kutoka kwa Mamar na Abu Hurayra kuwa Mtume (s.a.w) amesema: “Mtu anayeweka bidhaa kwa kutarajia kuwa bei zitapanda katika ardhi ya Kiislamu anatenda kosa.” (Haythami, ibid IV, 101 na at-Taj, Buyu, 2). Pia kuna hadithi zinazoeleza kuwa Allah atawatupia walanguzi Motoni. (angalia Haythami, ibid IV, 101)

2- Kukatazwa kupanga bei rasmi: katika uchumi wa Kiislamu, bei zilizopangwa, ukomo wa bei za juu na ukomo wa bei za chini usiwekwe. Ni haramu kupanga bei kwa mujibu wa rai ya wanazuoni wengi. Hata hivyo, imamu Malik anasema inaruhusiwa. Hata hivyo, lengo la kupanga bei ni kuzuia nguvu za mlanguzi anayezidisha bei katika soko kwa kuamua bei inayofaa. (Mansur Ali Nasif, Taj, II, 204, tanbihi: 4)

Mtume (s.a.w) hakuzingatia kuwa dola kupanga bei ndio njia ya kuzuia mfumuko wa bei. (angalia Fazlurrahman, İslamiyet ve İktiadi Adalet meselesi, (trans: Yusuf Ziya Kavakçı) s. 42). Ömer Nusuhi Bilmen anasema dola isipange bei na kuamua bei za bidhaa. Kuna hekima katika kila tendo la Allah. Kama ambavyo wakati mwingine bei hushuka na wakati mwingine hupanda kimaumbile, inatakiwa izingatiwe kuwa ni jambo la kawaida. (Ö.N.Bilmen, Istılahat-ı Fıkhiyye, VI, 125) Kwa upande mwingine, kupanga bei maalumu kunaweza kuwafanya watu wafiche bidhaa zao katika maisha ya kibiashara. Kuficha bidhaa husababisha bei zipande. Kupanda kwa bei kutawaumiza masikini. (Sayyid Sabiq, Fiqhu’s Sunnah, III, 105)

Imesimuliwa kutoka kwa Anas na Muhammad b. Abdurrahman kuwa mara moja bei zilipanda katika wakati wa uhai wa Mjumbe wa Allah (s.a.w). Watu wakamwendea Mtume na wakamwomba apange bei. Hapo, Mjumbe wa Allah akasema:

“Allah ndiye anayepanga bei, anasababisha wingi au uhaba na anatoa riziki. Ninaapa kwa Allah kuwa siwezi kukupeni wala kukuzuieni chochote kwa ruhusa yangu. Mimi ni mtunza hazina tu; ninafanya lile ninaloamrishwa kulifanya; Allah ndiye mtoaji. Ninataka kumfikia Allah bila ya kukiuka haki za yeyote kuhusu mali zao, maisha yao na damu.” (Abu Yusuf, Kitab-ul Kharaj, uk. 91; Abu Dawud, III, 272; Tirmidhi, III, 605; Ibn Majah, II, 741) 

3- Mojawapo katika yaliyokatazwa katika uchumi wa Kiislamu ni kushindanisha bei za juu ili kuwaghilibu wanunuzi. Hilo husababisha mfumuko wa bei, na kuleta hali inayomnufaisha muuzaji na dhidi ya mnunuzi. Mtume (s.a.w) amewakataza watu kutokufanya najash. (Bukhari, III, 91; Ibn Majah, II, 733; Tajrid, VI, 457). Najash inamaanisha kujifanya mnunuzi na kupandisha juu bei ya kitu ingawa mtu huyo hataki kununua ili kuwahimiza wengine wakinunue na kuzidisha bei yake. (Marghinani, al-Hidaya, III, 40; Kasani, V, 233; Ibn Qudama, al-Mughni, IV, 160; Molla Khusraw, Durar, II, 177) Baadhi ya wanazuoni wanaizingatia najash, inayoleta faida haramu, kuwa ni makruhu kabisa (makruh tahrimi) (Muhammad b. Abdurrahman ad-Dimashqi, Rahmat-ul Ummah, II, 2); wengine wanaeleza kuwa si halali. (angalia Ibn-ul Humam, Fath-ul Qadir, V, 240)

4- Hakuna ushahidi katika Quran na Sunnah wa kupanga kiwango cha faida. Kwa hakika, kiwango cha faida kipo katika bei inayojitokeza mahali ambapo usambazaji na mahitaji hukutana. Haifai kwa mfumo unaotumia soko huria kupanga bei na kuweka kiwango cha faida. Kwa hivyo, hakuna tarakimu inayohusu faida katika aya na hadithi. Ni jambo la kawaida kwa bei kupanda kama mahitaji yataongezeka lakini isifikiriwe kuwa faida kubwa sana ni halali katika Uislamu. Kiwango cha kimaadili cha jamii, msawazo wa usambazaji na mahitaji, tofauti ya mahali na wakati na sababu nyingi nyingine huathiri kiwango cha faida. Baadhi ya wanazuoni wanasema faida ni katika kiwango cha nusu ya bei (Ö.N.Bilmen, Hukuku İslamiyye, VI, 120); baadhi ya wanazuoni wanataja kiwango cha 1/ 2 na 1/3 katika kupanga bei. (Angalia Celal, Yeniçeri, Yıllık, uk. 212) Pindi faida katika miamala ya murabaha ni kama kiasi cha mtaji, Abu Hanifa hazingatii kama inaruhusiwa kupata faida tena wakati wa kuiuza. 

5- Katika hadithi hakuna upangaji kiwango cha faida lakini kuna mifano kadhaa inayotupa baadhi ya dhana kuhusu jambo hilo. Kama vile, Mtume (s.a.w) alipompa Hakim b. Hizam dinari 1 ili kumnunulia mnyama wa kumchinja sadaka. Hakim alinunua kondoo kwa dinari 1 na kisha akamuuza kwa dinari 2. Kisha, akamnunua kondoo mwingine kwa dinari 1 na akampa Mtume yule kondoo pamoja na ile dinari 1 nyingine. Mtume aliitoa ile dinari I kwa kuwapa maskini kama sadaqa na akamwombea dua Hakim awe na biashara nzuri. (Abu Dawud, III, 256; No: 3386) Tukio kama hilo lilifanyika baina ya Hz. Mtume na Urwa al-Bariqi. (Angalia Abu Dawud, III, 256; No: 3384) Katika hadithi zote mbili, tunaona kuwa kitu cha dinari 1 kiliuzwa kwa dinari 2 kwa faida ya asilimia mia moja. Maana yake, kwa faida iliyo sawa na mtaji.

Kuna hadithi nyingine kuhusu uhusiano baina ya mtaji na kiwango cha faida. Mtume (s.a.w) amesema, "Faida ya bidhaa ambazo hazikufidiwa na kufanyiwa kazi si halali. (Abu Dawud, III, 283, No: 3503; Ibn Majah, II, 737, No: 2187; Imamu Shafii, al-Umm, III, 70; Sarakhsi, Mabsut, XIV, 36). Maana ya faida ambayo haikufidiwa na kufanyiwa kazi huenda ikawa ni faida isiyo na urari wa faida-hasara, maana yake, isiyo na hatari. Sarakhsi (Sarakhsi, XV, 130–131; cf. Kasani, Badayi, IV, 206; Ibn-ul Humam, Fath-ul Qadir, V, 215, 265) anaeleza hilo kwa mfano ufuatao: mtu anakodi kitu kwa lira 100 na kisha anamkodisha rafiki yake au mtu mwingine bila ya kutumia gharama zozote au nyongeza yoyote kwa lira 120; hizi lira 20 ni faida ambayo hailipiwi au kufanyiwa kazi; yaani, haina hatari zozote. (angalia Kasani, IV, 206; Shawkani, Nayl-ul Awtar, V, 203 ff)

Kwa kuwa mtaji huwa na hatari zake na kama tutazingatia urari wa mtaji na hatari, tunaweza kusema chini ya nuru ya hadithi hapo juu na ijtihad ya Abu Hanifa kuwa kiwango cha faida mpaka kufikia kiasi cha mtaji kinaruhusiwa katika uchumi wa Kiislamu. Hata hivyo, hatumaanishi kuwa kuna kiwango na ukomo wa faida katika uchumi wa Kiislamu.

Kama tulivyoonesha hapo juu, faida ni kitu pamoja na shughuli kadhaa. Inaweza kuwa chini au juu kulingana na wakati, mahali na hali. Hata hivyo, kwa maoni yetu, kama faida imepatikana kutokana na kitu chini ya hali za kawaida ni zaidi ya mtaji wa kitu hicho, kiasi cha ziada, ambacho ni sehemu ya faida juu ya asilimia mia moja si halali.

6- Umuhimu mkubwa hupewa soko katika uchumi wa Kiislamu. Mtume (s.a.w) amesema yafuatayo kuhusu kutokuuza bidhaa njiani kabla ya kufika sokoni: “Msikatishe bidhaa za kibiashara katika njia ya kwenda sokoni…” Wanazuoni wa Kiislamu wamechunguza sababu za Mtume kukataza jambo la kukatisha bidhaa njiani na wakatoa maelezo kuhusu mmiliki wa bidhaa, wauzaji wa sokoni na watu wa eneo husika.

Huenda mwenye bidhaa akauza bidhaa zake kwa bei rahisi kabla hajafika sokoni kwa kuwa hajui bei na anaweza kupata hasara. Kwa hivyo, kama baadaye atafika sokoni, akaona kuwa bei ziko juu na kugundua kuwa ameghilibiwa, anaweza kutaka arejeshewe bidhaa zake na kutangua muamala. Wauzaji wa sokoni wasioweza kwenda nje ya mji ili kununua bidhaa kabla hazijafika sokoni watalazimika wanunue bidhaa hizo kutoka kwa wale waliozikatisha njiani; hivyo, watazinunua kwa bei ya juu na watapata hasara. Wale wanaozikatisha kabla ya kufika sokoni wataziuza kwa bei ya juu na watasababisha watu wa eneo hilo wapate hasara. Kwakuwa, kama wazalishaji wangefikisha bidhaa hizo sokoni, wangeziuza wenyewe moja kwa moja bila ya madalali na bei zisingekuwa za juu. (Imam Malik, Muwatta, IV, 307; Shafii, al-Umm, III, 93; Kasani, V, 232; Marghinani, IIı, 40; Ibn Taymiya, al-Hisba, uk. 11; Ibn Qayyim al-Jawziyya, at-Turuq-ul Hikamiyya, uk. 283; Ibn Humam, V, 239; M. Khusraw, II, 177; Ibn Nujaym, VI, 108; Shah Waliyyullah, Hujjatullah, II, 110; Sayyid Sabiq, Fiqh-us Sunnah, III, 11)

7- Kuna hadithi nyingine inayosaidia soko huria. Mtume amesema, “Watu wa mjini hawatakiwi kuuza bidhaa ya mwanakijiji kwa niaba yake.” (Bukhari, III, 94; Muslam, V, 17; Abu Dawud, III, 269) Basi, watu wa mjini wasiuze bidhaa za watu wa vijijini na wageni kwa niaba yao. Pindi Ibn Abbas alipoulizwa kuhusu maana ya hadithi hii, alieleza kama ifuatavyo: “Msijifanye madalali wao.”

Tunataka kutoa maelezo yafuatayo yanayotokana na Shafii: Wageni huleta bidhaa zao sokoni bila ya kulijua soko. Watu wanaoishi katika eneo hilo wanahitaji bidhaa. Hata hivyo, wenye bidhaa wanahangaika kupafikia mahali husika, kubeba bidhaa zao, n.k. Watu wanataka kuzinunua kwa sababu wanazihitaji. Kwa hivyo, wenyewe wanataka kuziuza haraka. Hivyo, bidhaa hizo zinauzwa baada ya kupatikana bei za soko, kwa bei inayofaa inayotegemea msawazo wa usambazaji na mahitaji. Kwa hivyo, wauzaji na wanunuzi wataridhika.

Kama tutachukulia kuwa watu wa mjini wanaziuza bidhaa hizo, madalali watazinunua kwa bei ya chini na kisha kungojea bei za soko zipande na kuziuza kwa faida ya juu. Hivyo, watawadhuru wenye bidhaa kwa kuwazuia kuziuza kwa bei inayofaa na watu wa eneo hilo kwa kulimbikiza bidhaa na kisha kuziuza kwa bei za juu. Kwa hali hiyo, pande zote mbili zitadhurika; kwa hivyo, Mtume amekataza mwamala wa namna hiyo. (Shafii, al-Umm, III, 92; Ibn Qudama, IV, 162; Ibn Qayyim, uk. 308)

8- Biashara mojawapo aliyokataza Mtume (s.a.w) ni kutaka kulipa bei ya juu kwa bidhaa ambayo mnunuzi na muuzaji wameshakubaliana kuuza na kununua. Mjumbe wa Allah amesema, “Msijaribu kununua kitu ambacho wawili wameshapatana. Ndugu yako anapotaka kununua kitu, usijaribu kukinunua kwa kulipa bei ya juu.” (Bukhari, III, 90; Muislamu, V, 12; Abu Dawud, III, 269)

Kwa mujibu wa hadithi hii, ni haram kuingilia biashara ya wawili waliokwishapatana na kuibatilisha. Ni haramu kumpa muuzaji bei ya juu kwa kitu ambacho amekubali kumuuzia mtu mwingine na kumwomba kuiacha biashara hiyo. (Marghinani, III, 90; Molla Khusraw, II, 177; Ibn Qudama, IV, 161; al-Ayni, Umdat-ul Qari, XI, 257; Ibn Humam, V, 239; Ibn Nujaym; al-Bahr, VI, 107; ash-Shawkani, V, 189)

9- Imekatazwa kuuza bidhaa kabla ya mtu kuzipata kwa sababu itasababisha bei nyingine mbali na inayotokana na bei ya soko. Mtume (s.a.w) amesema yafuatayo kuhusu jambo hilo: “Mnaponunua chakula, msikiuze kabla hamjakipokea.” (Ibn Majah, II, 749; No: 2226) Pia kuna maelezo yaliyosimuliwa kutoka kwa Ibn Umar. Wakati wa Mtume, watu walikuwa wakinunua nafaka kutoka kwa wafanyabiashara waliokuwa na misafara kabla hawajazipokea. Kisha, Mjumbe wa Allah akawatuma maafisa kwa wafanyabiashara. Aliwakataza kuuza nafaka kabla hawajazifikisha sokoni. Ibn Umar pia amesema kuwa Mtume alikataza kuuza nafaka zilizonunuliwa isipokuwa mpaka zikishapimwa na kupokewa. (Bukhari, III, 89; Muislamu, V, 23; No: 38; Nasai, VII, 287; Tajrid, VI, 437, No: 986) Ibn Umar aliongeza:

“Niliwaona baadhi ya walanguzi na walimbikizaji wakati wa Mtume. Walinunua chakula bila ya kupima na kupokea na wakataka kuwauzia wengine; walipigwa kabla hawajasafirisha bidhaa hizo na walikatazwa kuziuza bidhaa kabla hawajazipokea.” (Tajrid, VI, 446, No: 991) Hadithi hizi zilifafanuliwa kama ifuatavyo: kama mfanyabiashara anayeuza nafaka ataziuza kabla hazijafika sokoni, atasababisha bei zipande na kwa hivyo atawaumiza watu; kwa hivyo, ikakatazwa. (angalia Tajrid, VI, 437, Na: 986)

Mujazafa, maana yake, kuuza vitu bila ya kuvipima uzito na ukubwa, kwa maneno mengine, kununua vitu kwa jumla kwa mapatano, inazingatiwa kuwa ni halali. Hata hivyo, imekatazwa kuuza bidhaa zilizonunuliwa kama zile za kabla ya kuzipokea na kuzisafirisha kwa sababu ni namna ya biashara inayosababisha ulanguzi. Kama bidhaa zinazonunuliwa lakini hazijapokelewa zingeruhusiwa kuuzwa tena, basi baadhi ya bidhaa zilizowekwa ghalani zitapanda bei bila ya kutolewa na bila ulazima kwa kuuzwa tena na tena. Imeoneshwa na Ibn Umar kuwa inaelezwa katika hadithi kuwa ni lazima kupokea nafaka kabla ya kuziuza tena ili kuzuia kupanda kwa bei: Wenye bidhaa zinazofanyiwa mujazafa wanapigwa mpaka wazipakie nafaka hizo juu ya wanyama na kuzipeleka sokoni; inaelezwa kuwa kusafirisha bidhaa kutoka mahali zilipohifadhiwa kunamaanisha kuzipokea na kuzitoa, ambalo ndilo hitajio la Shari'ah ili kuzuia bei zisipande. Hili ndilo kusudio la hadithi. (Tajrid, VI, 447, 448)

9- Mtu asiyejiweza amekatazwa kununua na kuuza kwa sababu bei haitaendana na soko huria na itakuwa biashara iliyofanyika kwa sababu ya wajibu. Inaelezwa katika vyanzo kuwa aina hii ya kununua na kuuza, inayoitwa bay' al-muztar (kuuza au kununua ambako kumelazimishwa) ni haram. Inaelezwa katika hadithi iliyosimuliwa na Ali kuwa Mtume amemkataza mtu asiyejiweza kununua na kuuza. (Abu Dawud, Sharh Khattabi, III, 676)

Muuzaji anapouza bidhaa zake kwa mtu asiye na matumaini, atakiwa kumuuzia kwa bei ya kawaida bila ya kuzidisha; vinginevyo, ununuzi huu hautakuwa halali. (Ibn Abidin, IV, 110) Mtu anayepata kitu anachokihitaji tu katika sehemu moja, anahitaji kukinunua kwa bei ya kawaida. Muuzaji anatakiwa akiuze kwa bei ya kawaida hususani kama ni chakula au nguo ambazo mtu anapaswa kumuuzia. Ni wa wajibu kidini kwake kukiuza kama hivyo. (Ibn Taymiya, Fatawa, XXIX, 361)

Sasa, ninataka kunukuu baadhi ya kanuni kutoka katika kitabu changu, ambacho kilitayarishwa kama tasnifu ya udaktari, kinachoitwa “Kur'an-ı Kerim'e Göre İslam Ekonomisinin Esasları (kanuni za Uchumi wa Kiislamu Kwa mujibu wa Quran)”. Idadi kadhaa ya sura na aya zimewekwa katika mabano. Ni lazima kurejea katika sehemu inayoitwa Ushahidi na Maelezo ya nyenzo za kutafsiria aya.

Watu wameumbwa na kuelimishwa na Mola Mlezi mmoja. (2/139) Watu hawawezi kujiwekea wenyewe mfumo. Wanatakiwa kutafuta, wajifundishe na kutumia mfumo wa asili. (1/7) Mwanadamu ni chombo cha dola; kwa upande mwingine, ni kiumbe anayejitegemea anayeendeleza hadhi yake. (2/ 30) Hakuna anayeweza kunyimwa hadhi. (2/ 30) Mtu mmoja mmoja anaikabili dola moja kwa moja bila ya kutumia mshenga yeyote. (1/ 5)

Maisha ya kiuchumi ni maisha ya kimaumbile. Uingiliaji bandia katika maisha ya kiuchumi utayaharibu. (28/ 78) Lengo la shughuli zote za kiuchumi ni kuongeza idadi ya watu na bidhaa. (2/ 155)  Maendeleo ya kiuchumi hupimwa kwa kiasi cha bidhaa na idadi ya watu. (9/ 69) Tabia ya kiuchumi hujiunda katika mfumo kutokana nao. Mwenendo mwema hautoshi; mfumo mzuri ni muhimu. (2/188) Akili ya kibinadamu inaweza kupata mfumo utakaotenganisha heri na shari, na bidhaa mbovu na bidhaa nzuri. (5/100) Ni wajibu wa dola kuweka mfumo. (1/1) 

Uislamu una mfumo wa kiuchumi. (2/ 1–5). Biashara binafsi na biashara huria ni lazima katika Mfumo wa kiuchumi wa Kiislamu. (2/ 286) Mifumo ya biashara binafsi na ushindani huria ni matokeo ya kimaumbile ya mabadiliko na uchaguzi wa kiuchumi. (3/ 140) Katika uchumi wa Kiislamu, dunia na ahera, maada na hali ya kiroho hupewa umuhimu unaolingana. Kimojawapo hakiwezi kutolewa mhanga kwa ajili ya kingine. (24/ 37) Hakuna amri inayokosekana katika Quran. (6/ 38) Mambo mengi yamesimuliwa kwa njia ya mfanano katika Quran. Jambo husimuliwa moja kwa moja au kupitia linalofanana nalo. (6/ 38) Mfumo wa Kiislamu haukubali riba. (2/ 278) Zakah-kodi ni kinyume cha riba. (2/ 280) Mfumo wa riba huria na mfumo wa zakah ni mifumo miwili inayopingana. (30/ 39) Baadhi ya sehemu za mfumo na amri haziwezi kutumika kwa kutenganishwa na sehemu zingine kuachwa; huzingatiwa zote kwa ukamilifu wake. (2/ 208)

Uzalishaji wa kimsingi ni mimea ya kijani inayohifadhi nguvu ya jua. (6/ 99) Uzalishaji wa kimsingi ni mazao ya ardhi. (6/ 99) Mfumo wa uzalishaji unategemea mzunguko wa maji yanayodondoka juu ya ardhi kutoka angani. (14/ 32) Mito inatoa mchango mkubwa katika uzalishaji. (14/ 32) Ardhi na mbingu, hewa na jua, udongo na maji vinashiriki pamoja katika uzalishaji. (14/ 32) Jua, mwezi, mchana na usiku ni nyenzo za uzalishaji; na huzalisha bure kwa ajili ya watu kimaumbile. (14/ 33) Uzalishaji na kwa hivyo utumiaji ni wa kijamii (wote). Kila mmoja anapaswa kutenda kulingana na hayo. (1/5) Vitendo vya uzalishaji, utumiaji na kubadilishana vitendo ni mambo ya kijamii. (2/ 274) 

Dola ya Kiislamu haitofautishi baina ya raia Waislamu na wasio Waislamu kuhusu mambo ya kidunia. (3/110) Mali inamilikiwa na Allah; mtu mmoja mmoja ana haki na mamlaka ya kuitumia mali kwa niaba ya Allah. (2/ 180) Dola sio shirika la kijamii au la kibiashara lililoanzishwa na matajiri pekee; hivyo, masikini pia wanufaishwe na mapato ya dola. (59/ 7) Mapato yasiyo halali, bidhaa zilizofichwa na bidhaa haramu hayako chini ya dhamana ya dola. (2/ 270) Uvukaji mipaka katika mali binafsi unamaanisha kuvuka mipaka katika mali ya dola. Dola ina kazi ya kulinda mali zote. (3/ 26) Rais anaiwakilisha dola. (4/ 59) Wajibu wa mtu mmoja mmoja ni kuiweka serikali kwa kuitii. Haiwezekani kuongoza bila ya a serikali. (3/ 104) Serikali hutumia amri zinazoamuliwa kwa maafikiano. (4/ 59) Serikali hutunza na kuamuru na kufanya yaliyo mema. Serikali haziwezi kupanga bei. Hata hivyo, zinaweza kutaja bei zainazojileta zenyewe.. (3/ 104)

Serikali hazina haki na mamlaka ya kukusanya kodi ya ziada (2/ 272) kuongeza viwango vya kodi (3/ 161) na kuweka kodi mpya. (3/ 161) Mtu asiwaonee husuda wale wenye mali na wenye uwezo. (4/ 53) Mali na serikali hupewa wale wanaostahiki zaidi. (4/ 58).

Mirathi ni haki halali katika uchumi wa Kiislamu. (4/7) Mfumo wa mirathi uliowekwa na watu unatofautiana na mfumo anaoamrisha Allah. Mfumo wa mirathi wa Kiislamu una faida nyingi kwa upande wa uchumi. (4/ 11) Sababu za kurithi ni undugu, ndoa na ulezi. (4/ 8) Suala la kuchukua mtoto wa kupanga na kurithi kwa njia hiyo haiwezekani. Mtu hawezi kuteuliwa kuwa mrithi. (4/ 33) Mali ya mtu asiye na warithi hupelekwa hazina. (4/ 8)

Kufanya kazi kunamaanisha kushughulika kwa kusudio na kutumia nguvu. (2/ 204) Kazi ni uwezo na nguvu inayomfanya mwanadamu akimbie, afanye jambo na kusogea. Kazi ni manufaa na inamilikiwa na mfanyaji. Chanzo cha mali ni kazi. (53/ 39) Kazi si mali; kwa hivyo, mabadilikobadiliko ya usambazaji na mahitaji hayatumiki katika kazi ili kuendeleza urari wa mishahara kama ilivyo katika mali. (2/ 148) Wafanyakazi wa watu wanatofautiana. (92/ 4) Tofauti ya nguvu na uwezo baina ya watu huwezesha kubadilshana kazi (ajira) kutambuliwa. (43/ 32) Kazi, ni dhahiri kuwa kutakuwepo ugawaji kazi katika maisha ya kibiashara. (92/ 4) Viwango vya kazi zenye vigezo na zisizo na vigezo zinatofautiana. (6/ 132)

Mfuko wa kwanza katika biashara, mkopo na mambo mengine yanaitwa mtaji. (2/ 279) Katika Uchumi wa Kiislamu, mtaji una sheria mbalimbali; kwa hivyo, inawezekana kugawanya mtaji katika sehemu mbili ambazo ni mtaji wa kudumu na mtaji unaozunguka. (2/267) Si sahihi kutaka usawa wa watu kwenye mali na mtaji, kudai kuwa watu wako sawa na kuchukulia kuwa mtumwa na bwana wake wako sawa. (30/ 28) Zakah huweka mipaka ya juu kwenye mitaji; hivyo, ulimbikizaji uliokithiri wa mtaji umezuiwa na wenye mtaji wanashurutishwa kuwekeza. (2/ 276) Hakuna usawa wa ugawaji na uzuiaji mali katika jumuia. (3/ 35) Pindi mkopo unapotolewa kwa anayefanya kazi, hakutakuwa na utumiaji mbaya wa mtaji. (2/ 245) katika ubia wa mudharaba, mwenye mtaji hupata hasara. (2/ 267)

Bidhaa zinamaanisha kuwa Allah amewaumba watu ili wakidhi mahitaji yao duniani. (2/ 155) Bidhaa humwezesha mwanadamu kutimiza mahitaji yake, kukimu maisha yao, kudumu na kuwa ni mtawala duniani. Bidhaa ni vitu ambavyo maumbile ya mwanadamu yanavitaka na vinavyoweza kuhifadhiwa kwa ajili ya mahitaji ya baadaye. Kwa maneno mengine, bidhaa ni vitu vinavyoweza kununuliwa na kuuzwa, vyenye thamani na vinavyotaka kulipiwa na anayeviharibu. Kutokana na hayo, vitu kama mwangaza wa jua, nguvu ya jua na hewa vina manufaa sana lakini haviwezi kuzingatiwa kuwa ni bidhaa kwa sababu haviwezi kuhifadhiwa. Hata hivyo, gesi iliyojazwa kwenye mitungi huzingatiwa kuwa ni bidhaa kwa sababu imehifadhiwa. (4/5) Anachopata mwanadamu kwa kufanya kazi, anachokipata na kukitumia hitwa bidhaa. Kodi hutozwa juu ya vitu kama hivyo (kama vile, lami, petroli, mawe, metali zenye kuyeyuka na zisizo yeyuka, n.k) (2/ 272) Bidhaa ni za kimataifa na huzunguka baina ya mataifa. Ni lazima kuhakikisha mzunguko wa bidhaa na pesa baina ya matabaka yote. Bidhaa zina manufaa sana kwa wenye kuzihitaji zaidi. Kuna madhara pindi bidhaa na pesa zinapozunguka mikononi mwa matajiri tu. (59/ 7)

Haki ya mali kwa mtu inamaanisha kuwa na haki na mamlaka ya kumiliki bidhaa na vitu vinavyozingatiwa kuwa ni bidhaa na kuzitumia kwa uhuru kwa ajili ya manufaa yake mwenyewe. (3/ 26) Mali ni kitu cha muhimu na sifa ya kuwa binadamu. (9/ 34) Kila kitu ni kwa ajili ya mwanadamu; hakuna kiumbe mwingine mwenye haki ya kumiliki mali. (2/ 29) Mfumo wa mali ni mfumo wa dola nayo ni rehema kwa ajili ya watu. (4/ 29) Mfumo wa mali ni wa wajibu kwa mtu mmoja mmoja na jamii. Mtu mmoja mmoja anapaswa kutii mfumo wa mali madam anaishi katika jumuia. (2/ 180) Haki ya mali huwa chini ya mfumo wa kisheria. Kuiingilia mali ya mtu hairuhusiwi kamwe. Kupanga bei moja, kuweka fedha za kigeni na mikopo maalumu kamwe hakupo. Serikali haziwezi kuingilia kati uchumi isipokuwa kodi wanazotoza. (3/ 26) Mtu mmoja mmoja ana haki yenye mipaka yake katika mali. (3/ 26) Hakuna haki isiyo na mipaka katika mali bali yenye masharti katika uchumi wa Kiislamu. (24/ 33) Usawa katika mali na utumiaji si katika swali. (16/ 71) Si sahihi kutaka usawa kwa ajili ya watu kuhusu mali na mtaji. (30/ 28)

Katika mfumo wa uchumi wa Kiislamu, biashara binafsi na biashara huria ni lazima. (2/ 286) Kila mmoja anaweza kuchagua kazi yake mwenyewe na anajua kitu cha kuzalisha na namna ya kuzalisha. (2/ 148) Kazi hufanywa kwa kuzingatia mali binafsi na biashara binafsi, kwa pamoja na katika mfuatano. (2/ 110) Katika maisha ya kufanya kazi, mgawanyo wa kazi ni lazima. (17/ 84)

Mshahara ni malipo yatokanayo na kazi iliyotumiwa. Kodi ni malipo yatokanayo na kitu au huduma iliyotumiwa. (28/ 27) Ni halali kumwajiri mfanyakazi kwa ajili ya mshahara. (43/ 32) Urari baina ya faida na hasara, mshahara na kazi, kodi na mahali ni imara. Yanaunda urari baina ya hayo na mengine. (2/ 275) Mshahara hulipwa mfanyakazi sio kwa lengo la kumfanya aishi bali analipwa ili kufanya apate sehemu ya mtaji na kwa ajili ya kazi yake. (1/ 5) Mishahara hupangwa kwa kuzingatia uwezo wa kitaalamu, muda, elimu, uzoefu, uwezo na uchapakazi. (2/ 282) Mshahara hulipwa kama tu kilichofanyika kina manufaa. (65/ 6) Mtu asiyefanya kazi bila ya sababu yoyote hastahiki kulipwa mshahara. (6/ 158) Mkataba hauleti hakikisho la kupata mishahara; mishahara hulipwa baada ya kufanyika kazi. (65/ 6) Matumizi ya sheria zisizofaa za mishahara, mishahara ya kiasili na mfuko wa mishahara haifai. (28/ 27).

Faida hufidia hasara; ni kupanda kwa thamani ya bidhaa; ni tofauti ya bei. (2/ 275) Faida zinazopatikana bila ya hatari yoyote huzingatiwa kuwa ni riba. (2/ 275)

Kodi inamaanisha kuuza baadhi ya manufaa kwa ajili ya kupata pesa. Inaruhusiwa kukodisha mali na bidhaa zisizokwisha kama zitatumika kwa kiasi fulani cha pesa. Mfanyakazi anazingatiwa kujipangisha mwenyewe kwa kuuza kazi yake. Bidhaa zenye kwisha kama zitatumika haziwezi kukodishwa; kama vile, maji hayawezi kukodishwa, ng’ombe hawezi kukodishwa kwa ajili ya maziwa na mti kwa ajili ya matunda yake. Hizo sio bidhaa halisi; kwa hivyo, zinaweza kuuzwa tu. (28/ 27)

Riba inamaanisha kupata kitu kwa malipo ya kukopesha. (2/ 282) Riba ni kitu cha ziada kisichokuwa na chenye kulingana nayo. Riba huongezeka baada ya wakati fulani na kuwa mara mbili, mara tatu, n.k; riba imegawanyika katika sehemu mbili, fadhl (riba katika ziada) na nasia (riba juu ya mkopo). Riba ni haram kwa Waislamu wote. (3/ 130) Riba hupunguza uzalishaji, huzuia viwanda visifanye kazi na kuvisimamisha katika hatua fulani, na kusababisha migogoro. (30/ 39) Riba hupunguza ubadilishanaji bidhaa, huzuia mzunguko na hupunguza pato la taifa. (2/ 276) Wale wasiokubali kukatazwa riba huzingatiwa kuwa wameiasi dola ya Kiislamu. (2/ 279)

Mfumo wa riba hutafuna na kula pato la taifa. (2/ 275) Kwa kweli, pindi pato la taifa linapokua, mapato ya dola huongezeka, pia. (23/ 72) Kupata pesa kwa njia ambazo si halali na kuitumia kutapunguza pato la taifa. (5/ 42) Katika mfumo wa riba, pato la taifa litapungua; na katika mfumo wa zakah, pato la taifa litaongezeka. (30/ 39)

Katika mfumo wa uchumi wa Kiislamu, mmiliki wa mahali anapata kodi, mmiliki wa mtaji unaozunguka anapata faida na mfanyakazi anapata mishahara. (2/ 267) Ugawaji wa mapato umepangwa kiuadilifu katika jumuia. (2/ 134) Manufaa ya ziada yaliyopatikana kutokana na uzalishaji yanagawanywa katika kodi, mkopo, faida na mishahara inayotegemea shari'ah (mikataba). (3/ 73) Nchi zisizopanga ugavi wa mapato kwa uadilifu haziwezi kuendelea; zimegubikwa na hali ya kuanguka na kuporomoka punde. (2/ 134) 

Nchi zinazoweka mfumo wao wa kimaumbile zitakuwa katika wingi na ustawi. (7/ 58) Wasiwasi na matatizo vinaondoshwa katika mfumo wa kiuchumi wa jumuia ambapo mfumo wa kodi umepangiliwa vyema; ustawi wa uchumi huondoa taabu na mashaka. (2/ 274) Heri na ustawi huhifadhiwa; hayo ni amani ya milele dhidi ya starehe za muda mfupi. (3/ 92) Mali na ustawi, umasikini na ubahili ni mambo ya kijamii. Maendeleo ya jumuia ni kwa ujumla wake. (2/ 155) Ustawi hutokea kutokana na vitendo vya kawaida vya kiuchumi. (5/ 66) Ustawi ni matokeo ya hatua ya kihistoria. (1/ 7) Baada ya jumuia kustawi, wingi na ustawi huongezeka. (7/ 95) Juhudi za mtu mmoja mmoja hazitoshi kwa ajili ya uokovu, ustawi na furaha; nyenendo za kijamii na vitendo ni muhimu. (3/ 186) Uhamaji husababisha wingi na mali. (4/ 100) Ndoa huleta wingi na mali, pia. (24/ 32) Nchi zisizoweza kuanzisha mfumo wa kimaumbile au wanauharibu hupata njaa na umasikini. (7/ 95) Ni lazima kupambanua baina ya heri na shari, bidhaa mbovu na nzuri, na bidhaa halali na haramu ili kuhakikisha ustawi. (5/ 100) Matendo machafu kama vile vilevi, kamari, masanamu na bahati nasibu yatakapoondoshwa kutoka mfumo wa kiuchumi, ustawi wa kiuchumi utaongezeka. (5/ 90) Jamii zinazochukua hatua za dhamana ya kijamii na kutoa haki za madaraja ya dhamana ya kijamii hupata ustawi. (30/ 38) Haiwezekani kuhakikisha ustawi na amani katika jamii kama masikini hawapewi bidhaa zinazofaa, chakula na nguo. (3/ 92) Kama mfumo wa biashara usio na riba ulioanzishwa na Uislamu utatumika kikamilifu, duniani kutakuwa mahali pa neema nyingi kama Peponi. Kuacha mfumo wa biashara usio na riba kutaleta mateso. (5/ 66) Jamii zinazoruhusu  yaliyokatazwa na kukataza yaliyoruhusiwa haitaweza kupata ustawi na furaha. (16/ 116) Haiwezekani katika jumuia ambapo majirani hawasaidiani kuwa watapata ustawi na furaha. (107/ 1–7)

Matumizi kwa ajili ya starehe yanaitwa anasa. Inaruhusiwa kutumia bidhaa za anasa (bidhaa zinazotumika kwa ajili ya starehe si kwa sababu ni za lazima) chini ya masharti fulani. Anasa isimzuie mtu kutoa sadaka na kusaidia wengine, isimpe msukumo mtu kufanya mambo ya haramu kuhusu kupata pato, kutumia na kubadilishana, kusimpelekee ukosefu wa imani na hatari na isimzuie kuwa na imani na kutenda amali njema. (5/ 93) 

Ubadhirifu unamaanisha kuvuka mipaka na kufanya mambo yaliyovuka mipaka juu ya jambo. (25/ 67) Katika hali yake ya ujumla, ubadhirifu unamaanisha kuchupa mipaka na kvuka wastani. Ubadhirifu unaweza kuwa katika njia mbili: kufanya mno jambo (ifrat) na kufanya jambo kidogo mno (tafrit). Maana yake, kufanya jambo kidogo mno pia ni ubadhirifu. (4/6) Anasa na matumizi ya kujionesha hakuzingatiwi kuwa ni mahitaji. Dola hailipii matumizi haya. (2/ 215) Jumuia ina mamlaka ya kuangalia kama bidhaa zinatumika katika njia ya ustawi au zinapotezwa ama laa. (6/ 141) Kutumia mali juu ya mapambo na uzuri kunaruhusiwa madam mtu hafanyi ubadhirifu. (7/ 32) Katika matumizi, kujionesha, anasa na matumizi ya kupoteza ni haram na ni dhambi lakini hayajakatazwa. (2/ 215) Waumini huepuka ubadhirifu na kujionesha katika matumizi. Wao hushindana kutoa sadaka sio kutumia ovyo na kujionesha. (3/ 14)

Vitu vya manufaa vinavyoufaa mwili vimefanywa halali na vinaruhusiwa; vitu visivyoufaa na vyenye kuudhuru mwili vimefanywa haramu na vimekatazwa. (2/ 175) Chakula chenye kuunufaisha mwili na kuweza kumeng’enywa ni halali na chakula kinachoudhuru mwili na hakiwezi kumeng’enywa si halali. (5/ 88) Allah Peke Yake Ndiye Mwenye haki ya kulifanya jambo liwe halali na haramu. Hakuna anayeweza kuamua kwa hiari yake mwenyewe kuwa kitu fulani ni halali au haramu. (2/ 275) Ni makosa kuzingatia kitu halali kuwa ni haramu. Inazingatiwa kuwa ni dhuluma na ukatili kukataza kitu ambacho ni halali. (5/ 87) Kilicho haram ni kutotumia bidhaa na kazi inapolazimu. (10/ 59)

Miamala inayozidisha matumizi ya ukingoni na kuweza kuwa na thamani kama bidhaa, kazi, pesa na mkopo kwa jumuia ni halali; na inayovipunguza hivyo ni haramu. Njia haramu za kupata pesa kama rushwa, kusema uongo, riba, kamari, wizi, matumizi mabaya, utapeli, upotoshaji, ghiliba, ulanguzi na kuchukua nafasi ya uchuuzi wa bidhaa kutoka kwa wamiliki wake kama gamba la mti linavyojibagua kutoka katika shina na kupunguza manufaa ya ukingoni. (5/ 42)

Katika uchumi wa Kiislamu, mfumo wa leo wa bima umebadilishwa kwa desturi ya infaq (sadaka). Katika uchumi wa Kiislamu, maisha ya kila mmoja yamedhaminiwa. Licha ya hivyo, hakuna desturi inayohakikisha malipo ya utoaji zawadi. Mfumo wa Kiislamu wenyewe ni bima. Hakuna kabisa haja ya kuwa na kampuni ya bima. Katika uchumi wa Kiislamu, ukusanyaji na ugavi kodi, maana yake, bajeti yenyewe inahakikisha maisha ya raia wote. Shukrani kwa ufahamu wa mali, taasisi na utawala wa Kiislamu, maisha ya wanyama wote na mimea yamedhaminiwa. Sababu ya infaq ni ndoa, ndugu na mali. Nafaqa inamaanisha kukidhi mahitaji ya chakula, vinywaji, nguo na makazi. (2/ 215) Dola ihakikishe mahitaji makuu ya kila mmoja. (6/ 164) Bima ya maradhi na ulemavu imechukuliwa na desturi ya ndugu katika Mfumo wa Kiislamu. (2/ 83) Nafaqa si msaada unaotolewa na ndugu bali ni matumizi ya fungu la dola katika faida ya mtu mmoja mmoja. (6/ 164) Mtoto huzaliwa, huishi na kufa katika familia na jumuia. (4/1) Pindi mtoto anapozaliwa, wajibu wa kumtunza ni wa baba kwa upande wa nafaqa (chakula). (65/ 6) Ndugu wasioruhusiwa kuoana au ndugu wanaoweza kurithiana wanatakiwa kutunzana. (17/ 26)

Siasa za kijamii au dhamana ya kijamii, elimu ya umma, mfumo wa kufanya kazi na kuishi yote hayo yamepangwa katika mfumo wa dola. (2/ 83) Msaada wa kifedha kwa ajili ya mtu hukusanywa katika familia kwanza, na kisha mtaani anapoishi, wilaya, mji, mkoa na kisha katika dola na duniani. (4/ 36) Ni muhimu mtu kutoa kitu bora zaidi ili awe mtu mwema kweli na kupata heri. (3/ 92) Bidhaa na wanyama wanaochinjwa huelekezwa katika jumuia ili kuhakikisha dhamana ya kijamii. (5/ 97) Dola inasaidia familia kadhaa pamoja na watoto wadogo, mtoto na mama. (6/ 151) Dola huwasaidia wenye matatizo ya kifedha na kulipa madeni yao. (2/ 280) Kila mmoja anapaswa kuwasaidia masikini kimwili na kutoa sehemu ya mali yake. (2/ 270) Licha ya wajibu wa kimwili unaotolewa kwa dola, ni muhimu kuanzisha taasisi za hisani kwa ajili ya misaada ya hiari. Taasisi za hisani ya kiuchumi zimeasisiwa pamoja na taasisi za hisani ya kijamii. (2/ 177)

Msaada wa kifedha kwa wazee, wagonjwa, watoto na masikini ni shukrani. (2/ 83) Hakuna anayeweza kuufuta baada ya kumsaidia mtu au kumfadhili. Sababu za wajibu wa kuwasaidia wengine mmoja mmoja ni kwa kuwa ni ndugu, kuishi jirani, kufanya kazi katika sehemu moja, ujirani na kutembeleana. (4/ 36) Wazazi, ndugu, yatima, masikini na wasafiri ndio ambao huweka urari wa kijamii. (2/ 215) Masikini hupewa haki zao kutoka Hazina. (17/ 26) Nchi zinazochukua hatua za hifadhi ya jamii hupata ustawi. (30/ 38)

Sadaqa (kodi) ni kodi ambayo walipa kodi hulipa kutoka katika mali zao kwa ajili ya Allah kwenda katika dola ili wapewe masikini. Sadaqa ni haki ya mafukara na masikini; si zawadi, sadaka au msaada. Sadaqa wanayopewa mafukara na masikini ni kama malipo na mishahara wanayopewa maafisa na wafanyakazi. Masikini ni yule ambaye pato lake la mwaka liko chini ya matumizi yake ya mwaka. Fakiri ni mtu asiye na mtaji na mwenye haki ya kupewa msaada kwa ajili ya kupata mtaji wake. (9/ 60) Masikini ni mtu asiyeweza kufanya kazi na fakiri ni mtu asiye na mali. Masikini hupewa pesa kutoka katika Hazina ili kukimu maisha yao na fakiri hupewa pesa kama mtaji. (2/ 83) Ndugu (dhul-qurba) ni watu wenye kushika nafasi ya kuwaangalia ndugu walio dhaifu majumbani mwao. Wenye kuwauguza wagonjwa na wazee wanazingatiwa kuwa wako katika kundi hili. (8/ 41) Ndugu, masikini, wasafiri na wengine hupewa haki zao moja kwa moja kutoka Hazina. (17/ 26)

Kuombaomba kunaangaliwa kuwa ni jambo baya. Hata hivyo, hilo linaruhusiwa kwa watu wasiojiweza wasio na kitu cha kuponea. Ni wajibu unaokaribiana na faradhi kuwasaidia waombaji masikini na wasiojiweza. Waombaji hawatakiwi kuumizwa au kuudhiwa; hata kama hakupewa kitu, hatakiwi kufukuzwa au kukaripiwa. Kama atang’ang’ania kuombaomba basi si masikini, anaweza kukaripiwa. (93/ 9-10)