Uislamu ni nini? Unaweza kutoa maelezo ya kina kuhusu Uislamu?
Submitted by on Tue, 07/08/2018 - 15:35
Dear Brother / Sister,
UISLAMU NI NINI?
Maana ya Neno Uislamu Kilugha
Kilugha, Uislamu unamaanisha kujisalimisha, kunyenyekea na kutii. Dini hii ndio inaitwa Uislamu kwa sababu ni dini yenye msingi wa kusalimu amri za Allah na kuzitii.
Maana Yake Kiistilahi
Ni njia ya maisha, mfumo wenye misingi ya imani na matendo ya kuwafanya watu wapate furaha kamili duniani na ahera, iliyotumwa na Allah na kufikishiwa watu kupitia kwa mitume. Uislamu ni sheria ya kiungu inayowaongoza watu wenye akili kuelekea mambo mazuri kulingana na hiari zao.
Yaliyomo katika Uislamu
Maana ya Uislamu ni kujisalimisha: kujisalimsha kwenye amri na makatazo ya Allah. Uislamu hautakuwepo bila ya kujisalimisha kwenye hukumu za Allah. (Angalia al-An'am, 162 na an-Nisa, 65) Mwanadamu ni mja aliyeumbwa na Allah.
Kwa kuwa Allah amekizingira kila kitu kwa elimu Yake na kwa kuwa Yeye ana hekima, sharti la utumwa ni kujisalimisha Kwake. Sheria za uhai humshurutisha mwanadamu kujisalimisha kwa Allah kwa sababu Allah ndiye anayezijua zaidi sheria hizo na anamjua zaidi mwanadamu.
Ulimwengu na kila kilichomo ndani mwake hutii sheria za Muumbaji huyo. Kwa hivyo, dini ya ulimwengu wote ni Uislamu. Jua, mwezi na nyota, vyote hivyo vinafuata Uislamu. Kwa kuwa Uislamu unamaanisha kumtii Allah na kujisalimisha Kwake, tunaona kwamba viumbe vyote hivyo vinamtii Allah bila ya kuasi. Yaani, tunashuhudia kwamba vinajisalimisha na kwamba vyote vinafuata Uislamu.
“Je, wanataka dini isiyo kuwa ya Mwenyezi Mungu, na hali kila kilichomo mbinguni na katika ardhi kimesilimu kwa kumtii Yeye kikipenda kisipende, na kwake Yeye watarejeshwa?" (Aal-i Imran, 3/83)
Katika aya hiyo hapo juu, kujisalimisha kwa viumbe angani na ardhini kumetolewa kama mfano na mwanadamu ameambiwa yafuatayo: "Ewe Mwanadamu! Jisalimishe kama wao." Kama Ali (ra) anavyosema, "Uislamu ni utii na kujisalimisha." Mtu asiyejisalimisha kwa Allah hazingatiwi kuwa ni Muislamu. Mtu huzingatiwa kuwa ni mtumwa wa yule anayejisalimisha kwake. Uislamu ni alama na taswira ya imani. Je kujisalimisha bila ya imani, yaani, Uislamu bila ya imani unawezekana? Hata ikiwezekana, haikubaliki. Munafikuna (wanafiki) ni watu wanaojisalimisha bila ya imani. Leo, watu wanaojitambulisha kuwa ni Waislamu huku hawaamini kuwa ni lazima, hao hawajapokea hukumu za Allah kwa moyo na wanafuata itikadi (dini) zingine wanaingia katika kundi hili. Uislamu (kujisalimisha) thabiti, ni lazima kujisalimisha katika Sharia'ah ya Allah bila kusita, kikamilifu na bila ya masharti yoyote.
Kama mtu atajisalimisha kwa Allah kwa hiari yake mwenyewe, na akaishi kama Muislamu kwa kuuchagua Uislamu, ataishi kwa amani na kwa kutangamana na ulimwengu tangu alipojisalimisha kwa yule yule ambaye ulimwengu umejisalimisha kwake. Basi, mtu wa namna hiyo anakuwa mwakilishi wa Allah juu ya ardhi.
UISLAMU NI NINI?
Haiwezekani kufafanua maana ya dini ya Uislamu kwa kifupi bali kwa urefu. Maana yake pana inaweza kufanyika tu kwa ufafanuzi wa Quran na Sunnah kwa sababu yaliyo katika Uislamu na mipaka yake yanabainishwa na Quran na Sunnah. Uislamu unaweza kufundishwa kutoka katika Quran na Sunnah. Allah ameifanya dini hii kuwa kamilifu na pana kwenye vipengele vyote. Hakuna jambo lisilokuwa na ufafanuzi katika Uislamu. Imebainishwa iwapo jambo ni halali, haramu, makruh (lenye kuchukiwa), sunnah, au wajibu; hukumu ya kila tendo au imani imebainishwa. Katka Uislamu kuna hukumu mahususi kuhusu imani, ibada, siasa, masuala ya kijamii, uchumi, vita, amani, sheria na yote yenye kumhusu mwanadamu; au, msingi wa mujtahid kufanya hukumu ni Quran na Sunnah. Allah anaeleza rasilimali hii ya Quran kama ifuatavyo:
“Na tumekuteremshia Kitabu hiki kinacho bainisha kila kitu." (an-Nahl, 16/89 na pia angalia Yusuf, 111)
Wanazuoni ambao ni Mujtahid huwa wanahukumu masuala ambayo hukumu zake hazikufafanuliwa waziwazi katika Quran na Sunnah kwa kuegemeza maamuzi yao juu ya Quran na Sunnah.
Mtume (s.a.w) aliufafanua Uislamu kwa njia nyingi. Mmojawapo ni huu ufuatao:
"Uislamu umejengwa juu ya kanuni tano: Kushuhudia kuwa hakuna mwenye haki ya kuabudiwa isipokuwa Allah na kwamba Muhammad (s.a.w) ni Mjumbe Wake, kuswali, kulip zaka, kufanya Hajj na kufunga katika Mwezi wa Ramadhani." (Bukhari, Iman 1; Muislamu, Iman 22; Nasai, Iman 13; Tirmidhi Iman 3)
Hadithi hiyo hapo juu inaeleza kuwa Uislamu una misingi mitano. Tunachotakiwa kuzingatia ni ukweli kuwa misingi hiyo mitano ndiyo nguzo za Uislamu isipokuwa zenyewe peke yake haziundi Uislamu wote. Hatuwezi kusema kuwa nyumba huwa na msingi tu; halikadhalika, si sahihi kusema kuwa Uislamu una kanuni tano tu. Mwenye kusoma Quran ataona kuwa maadili, uchumu, masuala ya kijamii, amani, vita, wema, uovu n.k. ni mambo yaliyotajwa pamoja na kanuni hizo tano katika Quran. Uislamu una msingi na jengo. Msingi una kanuni hizo tano. Jengo lina hukumu zingine za Uislamu zinazohusu maisha ya kibinadamu. Wajibu wa Muislamu ni kuujua Uislamu wote kwa ujumla na kuutekeleza wote kwa ujumla.
Chini ya nuru ya hadithi maarufu hapo juu, tunaweza kugawanya misingi ya Uislamu katika makundi mawili: imani, iliyoelezwa kifupi kwa maneno ya shahada na amali njema, zilizotajwa kama amali nne kutokana na umuhimu. Uislamu ni imani inayoanzia katika kalima ash-shahada (maneno ya shahada) na kanuni za imani. Uislamu ni ibada inayojitokeza pamoja na swala, zakah, saumu na hajj. Hizo zinaitwa kanuni au misingi ya Uislamu. Sehemu zilizosalia za Uislamu ni jengo lililowekwa juu ya misingi hiyo. Mambo yanayounda jengo hilo ni mifumo ya kimaisha ya Uislamu: mfumo wa kisiasa, mfumo wa kiuchumi, mfumo wa kijeshi, mfumo wa kijamii,mfumo wa elimu, n.k. Uislamu pia una vibali ili kuhakikisha mamlaka yake. (Vibali vinamaanisha kwamba ni nguvu ya kuhakikisha kuwa sheria na amri za kimaadili zinatekelezwa; inamaanisha desturi zinazohusu ushurutishaji). Vibali hivyo ni jihad, kuamrisha wema na kukataza uovu, adhabu asilia na adhabu za kiungu anazotoa Allah duniani na ahera. Hivyo, Uislamu ni imani, ibada, mifumo ya kimaisha na vibali.
UISLAMU NI NINI?
Maana ya Uislamu ni hali ya mtu kujisalimisha kwa Allah kwa nafsi yake ya ndani na ya nje, kwa moyo na mwili, akili na dhamiri, matakwa na chuki, hisia na nia. Maana ya Uislamu ni kuokoa moyo wa mtu, akili, mwili, nafsi ya ndani na ya nje dhidi ya vyote isipokuwa Allah. Uislamu ni mfumo wa ujumla, mpango wa vitendo vya kibinadamu wenye kuamuru kwa njia ya sheria na ufunuo unaohusu vipengele vyote vya maisha na uliotangazwa na kufikishwa na Mtume. Wenye kuutii mpango huu watapata malipo na wasiotii wataadhibiwa. Uislamu ni ukamilifu wa hukumu zilizoshushwa na Allah, itikadi, ibada, maadili, muamalat (miamala) na yote yaliyo katika Quran na Sunnah.
Kinyume cha Uislamu ni Jahiliyya (ujinga). (Jahiliyya ni jina linalokusanya namna zote za ukafiri kama ndio imani na mtindo wa kimaisha. Maana yake ni ukafiri.) Ujinga ni dhahiri kabisa uko kinyume cha kila sehemu ya Uislamu. Kama Swahaba Umar anavyoeleza, "Wanapojitokeza wasiojua Uislamu na Ujinga, mafundo ya Uislamu hufunguka moja baada ya jingine." Uislamu ni kinyume cha Ujinga katika vipengele vyote kwa sababu kila sehemu ya Uislamu ni kazi ya ujuzi wa Allah inayokizingira kila kitu. Kila rai na mwenendo ulio kinyume na Yeye ni Ujinga kabisa kwa sababu ni kazi ya elimu ya mwanadamu yenye mipaka. Aidha, fikra na matakwa ya mwanadamu vinaweza kumwelemea na kuifanya wema uonekane kama uovu na shari kama vile ni heri.
"Je, wao wanataka hukumu za Kijahiliya? Na nani aliye mwema zaidi katika kuhukumu kuliko Mwenyezi Mungu kwa watu wenye yakini?” (al-Maida, 5/50)
Baadhi ya watu wanapoona uzuri na ukomavu katika matendo, mtindo wa kimaisha au baadhi ya mifumo ya baadhi ya watu wanaofuata njia ya Ujinga, wanakuwa na mashaka. Hayo ni kwa sababu jambo la Kiislamu wakati mwingine linaweza kuwepo kwa watu wenye mfumo wa Ujinga, pia. Jambo hilo la Kiislamu linaonekana zuri huko, pia. Mjinga hutwaa mfumo huo kwa sababu hajui ukweli wa Uislamu. Kama angejua ukweli, basi angefahamu kuwa tendo jema lisilo na ukamilifu aliloliona katika Ujinga ni la Uislamu na litageukia upande wa chanzo chake na asili.
Kuna Uislamu na Ujinga katika imani mbalimbali. Upo Uislamu na Ujinga katika maadili, siasa, mafunzo, vita, amani na masuala ya kijamii. Upo Uislamu na Ujinga katika masuala yote yanayomhusu mwanadamu, katika sheria na kanuni zote. Ujinga katika imani na ibada ndio ujinga wa hatari zaidi. Kwa hivyo, Allah anawasamehe watu wanaofanya baadhi ya matendo ya ujinga wakiwa na imani thabiti isipokuwa Hasamehe watu ambao imani yao na ibada zao ni za Ujinga hata kama wana maadili kamili ya Kiislamu.
"Hakika Mwenyezi Mungu hasamehe kushirikishwa, na husamehe yaliyo duni ya hilo kwa amtakaye.” (an-Nisa, 4/48)
Allah ameuleta Uislamu ukiwa kamili. Mtu anayeuchukua wote ni Muislamu. Mtu anayeuchukua baadhi yake na akaacha sehemu yake nyingine anachanganya Uislamu na Ujinga.
“Kisha nyinyi kwa nyinyi mnauwana, na mnawatoa baadhi yenu majumbani kwao, mkisaidiana kwa dhambi na uadui. Na wakikujieni mateka mnawakomboa, na hali kuwatoa mmekatazwa. Je! Mnaamini baadhi ya Kitabu na mnakataa baadhi yake? Basi hana malipo mwenye kutenda hayo miongoni mwenu ila hizaya katika maisha ya duniani, na Siku ya Kiyama watapelekwa kwenye adhabu kali kabisa. Na Mwenyezi Mungu si mwenye kughafilika na yale mnayo yatenda.” (al-Baqara, 2/85)
Ni lazima kila Muislamu atakasike dhidi ya desturi na kanuni zote za Ujinga na kuuchukua Uislamu wote.
Lengo la dini ya Uislamu
Hukumu zilizowekwa na Uislamu zinalenga furaha ya watu. Wenye kutenda kwa kufuata hukumu hizo watapata furaha kamili duniani na ahera. Uislamu unamfanya mtu apate furaha kwa kuboresha moyo wake, fikra na matendo. Kwa kuwa furaha ya jamii hutegemea furaha ya mtu mmoja mmoja, furaha ya mtu mmoja mmoja inamaanisha furaha ya jamii. Uislamu umeweka baadhi ya hukumu ili kufikia lengo hili. Zinaitwa hukumu za Shari'ah.
Hukumu za Dini ya Uislamu
Hukumu za dini ya Uislamu zimegawanyika katika makundi manne.
a) Imani (Hukumu zinazohusu imani): Ni hukumu zinazohusu masuala ambayo mwanadamu anahitaji kukubali au kukataa katika dini ya Uislamu. Hukumu hizi humfundisha mwanadamu anachotakiwa kukubali na kukataa. Kwa kuamini kanuni za imani, mwanadamu anachukua chakula chake cha kiroho, anatakasa moyo wake dhidi ya imani potovu na anapata thamani yake halisi.
b) Vitendo: Vitendo ni mambo anayoyafanya mwanadamu. Ni vitendo vinavyotakiwa kufanywa au kutokufanywa. Hukumu zenye kueleza amali gani zifanyike chini ya hali zipi na namna amali hizo kuwa ni amali zenye kufaa huitwa amali za kivitendo; mathalani, kuswali, kutoa zakah, kufanya jihad, kutafuta elimu.
c) Maadili: Hizi ni hukumu zenye kufafanua hali na vitendo, mitizamo na uhusiano wa Kiislamu na wa kibinadamu. Ni hukumu zenye kuhusu kuyapendezesha maadili na kuelimisha dhamira; mathalani, kutokutukana au kudanganya, mtu kutaka vitu ambavyo hutaka kwa ajili ya nafsi yake, kwa ajili ya wengine pia.
d) sheria [Muamalat (Miamala), Uqubat (Adhabu)]: Hizi ni hukumu zilizo nje ya masuala kama ya imani, maadili na vitendo binafsi na vyenye kuhusu kuongoza dola, utawala wa jamii, masuala ya kiuchumi, ndoa, talaka, mirathi, mambo ya kibiashara na kisiasa; kwa kifupi, ni hukumu zote zenye kuamua sheria na kanuni za dola ya Kiislamu.
Uislamu si sehemu tu ya maisha ya mwanadamu bali ni wote kikamilifu pamoja na vipengele vyake vyote. Uislamu umeyazingira na kuyaainisha masaa ishirini na nne ya mwanadamu na masuala mengine yote tangu kuzaliwa mpaka kufa. Uislamu ndio maisha yote ya mwanadamu. Ni wote kikamilifu pamoja na imani yake, ibada na sheria. Hauwezi kugawanywa au kuambatanishwa na kitu kingine. Haukubali kupunguzwa au kuongezwa, na ushirikina. Ni mfumo kamilifu uliokamilishwa na Allah.
Sifa Bainifu za Ujumla za Uislamu
1) Uungu: (Ni wa Mola Mlezi; hali ya kuwa mungu) Uislamu ni dini ya kweli na ya kiungu. Uislamu unategemea ufunuo. Malengo na madhumuni yake ni ya kiungu. Radhi za Allah ndiyo malengo ya msingi ya Muislamu. Chanzo na mtindo wa Uislamu ni wa kiungu, pia.
2) Ubinadamu: (Kutangamana na hali ya kibinadamu) Quran ilishushwa kwa watu, na mitume waliteuliwa kutoka miongoni mwa watu. Uislamu unampa umuhimu mkubwa mwanadamu na akili ya kibinadamu; na umeweka hukumu. Kwa mujibu wa Uislamu, mwanadamu aliumbwa juu ya ardhi kwa namna bora kabisa na kama mwakilishi; alifanywa kiumbe wa kipekee mwenye sifa muhimu ya kiroho; na ulimwengu umetiishwa kwake. Uislamu hauyapuuzi makundi yoyote yenye uwezo na nguvu. Unawaongoza wote hao kwenda kwenye kutengemaa, kazi na maendeleo. Kwa kushughulikia mizigo anayomudu kuibeba, mwanadamu anaendelea katika njia yake kwa amani, usalama na utulivu. Majukumu hayo yanatangamana na hulka ya mwanadamu. Yanaunganishwa na uthabiti wa moyo na dhamiri ya mwanadamu. Uislamu unalenga katika kustawisha hulka yake. Hukumu zote za Uislamu zimeelekezwa kwenye furaha ya duniani na ahera..
3) Upana na kuenea: Uislamu ni wa milele wa kuwepo daima, mpana wa kuwajumuisha watu wote na wa kina kirefu cha kujumuisha mambo ya duniani na nje dunia. Ujumbe na hukumu zake ni zinauhusu ulimwengu wote na wanadamu. Uislamu unapanga hatua zote za maisha ya mwanadamu, tokea kuzaliwa mpaka kufa na nyanja zote za kimaisha. Mafunzo ya Uislamu pia ni mapana. Upana huo hudhihirika katika imani, ibada, tafakuri, maadili na fadhila, na utaratibu na sheria.
4) Wastani na usawa: Uislamu ni dini yenye nguvu za kimsingi kama vile usawa, kati upole, haki na wastani. Ni njia ya kuepuka ubadhirifu na upungufu. Uislamu hauna mambo ya msimamo mkali. Haumwachi mwanadamu apotee na kukandamizwa. Uwezo wa mwanadamu hautoshi kuweka mfumo wa usawa. Tunaweza kuona kirahisi vipengele vya wastani (haki na usawa) katika imani, ibada, maadili na utungaji sheria. Kuna mizani kati ya dunia na ahera, maada na roho, tajiri na masikini. Uislamu huweka kwa usawa ndani na nje ya mwanadamu, roho na mwili, mtu mmoja mmoja na jamii, wanawake na wanaume, familia na taifa. Uislamu unapambanua haki zao kwa kila mmoja kwa usawa na utangamano.
5) Uwazi: Kanuni za imani na fikra za Uislamu ziko wazi na bayana. Ni nyepesi kuzifahamu, kueleza na kukubali. Hazikataliwi na akili na mantiki.
6) Dini Safi: Ni dini isiyoweza kuvurugwa kwa kuwa hairuhusu uchambuzi na usanisi (uunganishaji), kupunguzwa na kuongezwa na kwa kuwa chanzo chake ni kamili na kisichobadilika. Haiingiliwi na ushirikina. Ni dini pekee ya kweli iliyokamilishwa na kukubaliwa na Allah.
7) Upwekeshaji (Tawhid): Uislamu kimsingi ni dini ya upwekeshaji. Katika Uislamu ndiko kwenye kumwamini Allah kwa usahihi. Katika Islam, sifa za Allah haziwezi kuhusishwa na watu na viumbe wengine. Uislamu unasisitiza kuwa Allah hafanani na yeyote. Watu na viumbe wengine hawawezi kufanywa miungu. Haiwezekani kumwabudu yeyote mwingine isipokuwa Allah.
8) Kuwakubali Mitume wote: Muislamu anawaamini mitume wote waliotumwa na Allah. Hambagui yeyote miongoni mwao. Anawakubali kuwa ni wajumbe na waja wa Allah kwa kutokuwafanya miungu na kutokuwapa sifa za Allah wasizozistahiki.
9) Mamlaka ni ya Allah: Allah ndiye mwenye maamuzi, sheria na kanuni na kuweka sheria. Uislamu umejenga jamii ambapo hukumu, utawala, amri na mamlaka ni ya Allah na ambapo hakuna wenye kudhulumu, kudhulumiwa na watumwa wa watumwa.
10) Chanzo kamili: Chanzo kikuu cha Uislamu ni Quran. Quran ni kitabu ambacho hakitageuzwa-geuzwa mpaka Siku ya Kiama. Nakala zote za Quran duniani ni sawasawa.
11) Kutangamana na ulimwengu: Ulimwengu na kila kilichomo huzingatiwa kuwa kinafuata Uislamu kwa kuwa kinajisalimisha kwa Allah na kumtii. Mwenye kuupokea Uislamu na kujisalimisha, anatii kanuni zilezile katika kutangamana na ulimwengu. Hivyo, jitihata na nguvu za mwanadamu huunganika na nyezo za ulimwengu. Uislamu haumfanyi mwanadamu ashindane na kupigana na nguvu za asili ulimwenguni.
12) Uislamu unajenga jamii moja (umma): Uislamu unajenga jamii (umma) yenye utangamano na uaminifu na kutenda kwa mshikamano. Nguvu za msingi za jamii hii, inayounganishwa na kifungo cha imani na isiyobagua mbari, rangi, nchi na matabaka ni undugu, mshikamano, usawa, haki, kunasihiana ukweli na subira, kueneza heri na kupambana na shari. Ni jamii bora yenye maadili ambapo desturi mbaya kama vile uzinifu, ukahaba, wizi, dhuluma na riba vimeondshwa, ambapo matakwa yaliyovuka mipaka wa mwanadamu kwa ajili ya kula, kunywa, makazi na ngono umezuiwa. Makafiri hutazamwa kama ni umma mmoja; halikadhalika, Waislamu wote ni umma mmoja ambapo wao kwa wao huangaliana kama ndugu.
13) Wepesi na bishara: Uislamu humwangalia yeyote mwenye kutamka kalima ash-shahada na kuishi nayo maishani kuwa ni Muislamu pasi na kujali kuwa hapo nyuma alikuwa vipi. Uislamu umejikita juu ya kanuni ya usawa na haki. Haumruhusu yeyote kushurutishwa kuwa Muislamu. Unalenga katika kuenea kwa kuzishinda nyoyo. Hukumu zake ni nyepesi zinazoweza kutekelezeka. Mengi mepesi yamewekwa kuhusu ibada kwa kuzingatia ustahamilivu wa mtu (Mengi mepesi kuhusu ibada yameelezwa kuuchukua uthabiti wa mtu kwenda kwenye umakini). Majukumu magumu hayajaamrishwa na Uislamu. Kwa rehema ya Uislamu, ruhusa na bishara ni nyingi. Uislamu unaangalia mahitaji ya kiroho na kimwili ya binadamu kwa ustahamilivu na kuzitafutia ufumbuzi mwepesi na rahisi. Hata hivyo, wote wenye kupuuza kumwabudu na kumtii Allah licha ya wepesi wote huo kwa sababu ya uvivu na kuipenda sana dunia wanaonywa juu ya adhabu ya Allah.
14) Uislamu unaipa umuhimu the akili na elimu: Uislamu ni dini ya ufunuo lakini unaipa umuhimu akili. Uislamu pia unaipa umuhimu mkubwa sayansi na na elimu, kwa kueleza kuwa elimu ni faradhi kwa Waislamu wote; unayapa umuhimu masuala kama kazi, mafunzo na fikra. Isisahaulike kuwa Uislamu si dini ya kufikirika bali ya kiakili.
15) Haki za kibinadamu: Uislamu, ambao unajali haki za kibinadamu kwa namna ambayo hawataweza kuiona katika mfumo (dini) wowote mwingine, unalinda haki zifuatazo za mwanadamu:
a. Usalama wa dini: Uislamu unalinda haki ya dini na uhuru wa kuitekeleza dini.
b. Usalama nafsi: Uislamu unahakikisha haki ya kuishi.
c. Usalama wa akili: Uislamu, unaoamuru sayansi na tafakuri, unakataza vyenye kudhuru akili kama vile ulevi na madawa; unachukua kila hatua ili kulinda akili dhidi ya namna zote za kuchanganyikiwa.
d. Usalama wa kizazi: Unachukua hatua zote za lazima ili kuhakikisha adabu na heshima na makuzi ya kizazi chenye afya.
e. Usalama mali: Uislamu unaziba njia zinazoelekea kwenye uhalifu kama vile wizi ili kuhifadhi mali; zaidi ya hayo, humpa mwanadamu haki na fursa ya kuwa na njia za kutosha za kutafuta riziki.
Kwa ujumla, Uislamu unatoa dhamana kwa heshima, adabu, uhuru, dini, uhai, utafutaji riziki na kazi ya kila mtu.
Kuhusu suala la haki za binadamu, Uislamu bado upo katika kiwango cha juu sana ambacho hakiwezi kufikiwa. Unahimiza kanuni za undugu wa wanadamu. Uislamu unakataa ubaguzi wa kimbari na kutambua ubora wa mtu isipokuwa kwa taqwa (uchamungu). Amri za Uislamu, makatazo, hukumu, ibada, ufahamu wa adhabu, n.k vinahakikisha usawa. Kiasi hiki kikubwa cha usawa hakipo katika mifumo mingine hata kwa nadharia. Uislamu haujaacha kutilia maanani dhuluma kwa ajili ya usawa. Hauruhusu unyanyasaji wa kijinsia kwa kutoona tofauti za kijinsia kwa kisingizio cha usawa wa wanawake na wanaume na kuvuka mipaka kutakakopelekea kwenye kuwanyonya na kuwakandamiza watu. Kuhusu suala la haki za kibinadamu, Uislamu bado upo katika kiwango cha juu sana ambacho hakijawahi kufikiwa. Unahimiza kanuni za undugu wa wanadamu. Uislamu unakataa ubaguzi wa kimbari na kutambua ubora wa mtu isipokuwa kwa taqwa. Amri za Uislamu, makatazo, hukumu, ibada, ufahamu wa adhabu, n.k vinahakikisha usawa. Usawa wa kiasi hiki haupo katika mifumo mingine hata kwa nadharia. Uislamu haujaacha kutilia maanani dhuluma kwa ajili ya usawa. Haupuuzi tofauti za kijinsia kwa kisingizio cha usawa wa wanawake na wanaume na kuruka mipaka kutakakopelekea kwenye kuwanyonya na kuwakandamiza watu.
Uhusiano wa Uislamu na Shari'ah za Mitume Waliotangulia
a) Uislamu ni jina la dini zote zilizoshushwa kupitia kwa mitume wote. (angalia al-Baqara, 130 - 133). Utu uliletwa duniani na mtume (Adam). Allah aliwatuma mitume kuleta shari'ah (sheria) tofauti zilizoegemea mazingira ya wakati huo na mahitaji ya wanadamu; hata hivyo, imani ilikuwa ileile kwa mitume wote.
b) Dini zilizofikishwa na mitume waliotangulia zilipelekwa kwa baadhi ya mataifa. Dini aliyotumwa Mtume Muhammad (s.a.w) ni ya wote. Yaani, Allah aliileta ulimwenguni kote na kwa watu wote; ni njia ya maisha itakayokuwa halali mpaka Siku ya Kiama.
c) Dini ya Uislamu, aliyofikisha Nabii Muhammad (s.a.w), ilifuta hukumu (shari'ah) za dini zilizofikishwa na mitume waliotangulia. Yaani, iliyo hai kwa sasa ni shari'ah ya Nabii Muhammad (s.a.w).
d) Dini ya Uislamu inathibitisha vitabu vyote na mitume wote waliotumwa na Allah kabla ya Nabii Muhammad (s.a.w).
Baadhi ya Aya Zinazoeleza Uislamu
“Bila ya shaka Dini mbele ya Mwenyezi Mungu ni Uislamu.” (Aal-i Imran, 3/19)
“Na anaye tafuta dini isiyo kuwa Uislamu haitakubaliwa kwake. Naye Akhera atakuwa katika wenye kukhasiri.” (Aal-i Imran, 3/85)
“Na mwenye kuuelekeza uso wake kwa Mwenyezi Mungu, naye akawa anafanya wema, basi huyo hakika amekwisha kamata fundo lilio madhubuti. Na mwisho wa mambo yote ni kwa Mwenyezi Mungu.” (Luqman, 31/22)
“…Leo nimekukamiliishieni Dini yenu, na nimekutimizieni neema yangu, na nimekupendeleeni UISLAMU uwe ndiyo Dini....” (Al-Maida, 5/3)
Misingi ya Islam
Misingi (nguzo) za Uislamu ni mitano: Kushuhudia kuwa hakuna mwenye haki ya kuabudiwa isipokuwa Allah na kwamba Muhammad (s.a.w) ni Mjumbe Wake, kuswali, kulipa, kufanya Hajj na kufunga wakati wa mwezi wa Ramadhani.
Katika hadithi ambayo Mtume anafafanua Uislamu, inayojulikana kama hadithi ya Jibril, tuliyoitaja mwanzoni na inayoeleza kuwa Uislamu umejengwa juu ya nguzo tano (ambazo wajinga kimakosa huziita masharti ya Uislamu), nguzo hizo tano zimeorodheshwa. Tutashughulikia kanuni za msingi za imani tunazoziita kalima ash-shahada au kalima at-tawhid kwa kina tutakapoeleza suala la upwekeshaji (tawhid). Hapa, tutataja kwa kifupi kanuni (nguzo) zinazoeleza kama mifano ya kifani kutokana na umuhimu wa aina hizi za ibada na tunazoweza humo humo kueleza matendo hayo mema pamoja na ibada nyengine kama hizo zinazohusiana na imani. Namna ya kuzifanya ibada hizi imeelezwa kwa kirefu katika vitabu vya maswali na majibu na katika somo la fiqh.
Ni nini amali njema (amal salih)? Amali njema ni vitendo anavyovipenda Allah. Amali njema ina sifa mbili: Ya kwanza ni kuafikiana na shari'ah ya Uislamu; ya pili ni nia iwe kwa ajili ya Allah na kulenga kumwabudu. Kama amali haina sifa hizo mbili, haizingatiwi kuwa ni amali njema kwa Allah. Amali hiyo haina faida wala malipo. Mola wetu Mlezi anasema ifuatavyo:
“…Mwenye kutaraji kukutana na Mola wake Mlezi basi naatende vitendo vyema, wala asimshirikishe yeyote katika ibada ya Mola wake Mlezi..” (al-Kahf, 18/110)
Nafasi ya amali njema katika Uislamu ni muhimu sana kwa sababu vitendo hivyo ni matunda ya kumwamini Allah na akhera. Maana ya kalima ash-shahada (tawhid) inadhirika kwa kufanya matendo mema na kuendelea kufanya hivyo. Tunapokumbuka kuwa maana ya Uislamu ni kujisalimisha na utii, na kwamba kujisalimisha huko kunamaanisha kutii na kujisalimisha kwenye amri za Allah, inadhihirika wazi kuwa Uislamu hauwezi kuwa bila ya vitendo, utii na ibada. Aya nyingi zinasifu amali njema kutokana na umuhimu wake katika Uislamu. Baadhi ya aya hizo huzitazama kama ziko karibu na imani; baadhi hutaja malipo yake na nyingine hutaja manufaa yake katika akhera.
“Naapa kwa Zama! Hakika binaadamu bila ya shaka yumo katika khasara, Ila wale walio amini, na wakatenda mema, na wakausiana kwa haki, na wakausiana kusubiri...” (al-Asr, 103/1-3)
Kuhusu baadhi ya aya zingine, angalia al-Maida, 9 ; ar-Ra’d, 29 ;an-Nahl, 97 ; al-Kahf, 30; Maryam, 76; al-Ankabut, 7, 9.
Ni lazima kuufata Uislamu ili amali iweze kukubaliwa. Kwa hivyo, Allah anataja imani na amali njema kwa pamoja. Kama mtu atafanya jema lenye kufikiana na shari'ah ya Uislamu na kwa ajili ya Allah, jambo hilo litakataliwa na Allah isipokuwa akiukubali na kuufuata Uislamu wote kikamilifu. Amali hiyo haitakuwa na malipo. (angalia Aal-i İmran, 3/85)
Kuna namna nyingi za amali njema. Hayo ni mambo yote anayoamuru Allah, ambayo ama yanahusu ibada au miamala. Muislamu anapofanya jema kwa lengo la kumtii Mola wake Mlezi, anajisalimisha kwenye shari'ah na atakuwa anatafuta radhi za Allah, hapo atakuwa mtu wa amali njema.
Kwanza kabisa, matendo mema (kwa mtazamo finyu) ni matendo ya ibada. Vitendo vikuu vya ibada swala za kila siku, hajj na zakah. Hiyo ni misingi ya Uislamu. Hairuhusiwi hata kidogo kupuuza au kutweza umuhimu wake. Kwa hivyo, imeelezwa waziwazi katika hadithi mashuhuri zenye kuufafanua Uislamu.
Umuhimu wa ibada katika Uislamu ni mkubwa. Ibada huratibu uhusiano wa mtu na Mola wake Mlezi na kuonesha kumtumikia kwake Allah. Ibada ni haki maalumu ya Allah kutoka kwa waja Wake. Ni lazima kuchunga ibada na kuwaita watu wengine kwenye kanuni za imani na kisha ibada. Ibada isipokamilika, imani ya mtu haiwezi kuimarika na haitatulia moyoni mwake. Zaidi ya hivyo, leo hii, kwa vile mamlaka ya ukafiri yamefika kila mahali, imani ya watu wanaotekeleza ibada kivivu na kuacha baadhi ya ibada hususani swala za kila siku ni jambo la hatari. Yaani, ni vigumu sana mtu kundelea kuwa muumini bila ya kuswali na kufanya ibada nyengine. Ibada ni kama vile maji kwa samaki na hewa kwa mwaadamu.
Miongoni mwa ibada hizo, swala za kila siku zina umuhimu maalumu katika sharti la imani. Uislamu unaeleza swala kama sifa inayotofautisha kati ya Muislamu na kafiri. Hairuhusiwi kupuuza swala hata safarini, vitani, au mtu anapougua. Ni tabia ya wanafiki kuacha swala na kupuuza unapowadia wakati wa kuswali. Mtu anaporejea kwa Mola wake Mlezi, jambo la kwanza atakaloulizwa ni swala. Swala ni ibada ambayo mara kwa mara humkumbusha mtu kuhusu utumishi wake kwa Allah na maana ya kalima at-tawhid. Swala humzuia mtu kufanya vitendo vyote vibaya, uzinifu na uovu. Baadhi ya aya za Quran zinazohusu umuhimu wa swala ni hizi zifuatazo: ar-Rum, 31; al-Baqara, 1-3, 153 na 238; an-Nisa, 103; 142; al-Ankabut, 45...
Muislamu huitwa kwenye swala kwa tamko “Allahu Akbar”; anaanza swala kwa maneno hayo; anayakariri wakati anaposwali kwa sababu Allah ni mkubwa kuliko kila aliye mkubwa na Yuko juu kuliko kila mfalme mwenye nguvu. Kama mtu atasikamana na Allah, ambaye ni mkubwa na mwenye nguvu kuliko kila kitu, hatamwogopa yeyote. Ataacha kuwaabudu wengine.
Saumu, hajj, zakah na ibada zote zingine huimarisha imani, hutakasa roho ya uovu na kumfanya mtu amng’ang’anie Mola wake Mlezi. Katika saumu, mtu hutanguliza kumpenda Allah kuliko mahitaji ya mwili wake. Humfanya Muislamu awe mnyoofu, kuthubutu na matakwa na subira. Zakah ni ibada kwa upande wa mali inayomwezesha Muislamu kutakasika dhidi ya ugonjwa wa ubahili. Shukrani kwa nia ya zakah, anaifahamu vyema kuwa Allah ndiye mmiliki halisi wa mali na kwamba yeye amepewa dhamana tu ya mali hiyo. Zakah inamaanisha kutanguliza radhi na kumpenda Allah kuliko kupenda mali. Inamaanisha mtu kutenga fungu la mali yake na kuwapa masikini katika jamii na kwa hivyo kuchangia ustawi wa kijamii. Hajj ni mafunzo ya kivitendo kwa Muislamu. Tunaona kuwa Muislamu anatumikia kwa vitendo na waziwazi kwa njia ya ibada ya hajj. Maamrisho kama vile kutafuta elimu, kufanya jihad, kuamrisha wema, kukataza uovu, kuwa na subira na tawakkul, kuwa na taqwa, kumpenda Allah na kuhofu adhabu Zake ni katika matedo mema yanayosisitizwa sana katika Quran.
Kufikisha ujumbe wa Uislamu
Uislamu lazima ufikishwe kwa kila mmoja kadiri mwanadamu anavyokuwepo. Lengo halisi la kulingania na kufikisha ni kuwaokoa watu dhidi ya kuwa watumwa wa watu wengine na kuwafanya wamwelekee Allah peke yake, ambaye ni Mmoja. Lazima kila mara kuwe na watu wenye kutekeleza wajibu huo.
“Na uwe kutokana na nyinyi umma unao lingania kheri na unao amrisha mema na unakataza maovu. Na hao ndio walio fanikiwa.” (Aal-i Imran, 3/104)
Aya hiyo inathibitisha wajibu huu. Uislamu lazima ufikishwe kwa kila mtu lakini hususani kwa wenye kutenda matendo ya kijuujuu kama Waislamu kwa sababu wanaouona kama Uislamu si Uislamu halisi. Hali hii lazima ibadilishwe kabisa na waoneshewe ukweli.
Lengo mojawapo la kuwaita watu kwenye Uislamu ni kuunusuru usihodhiwe na watu wasiomfikishia yeyote na kumjulisha kila mmoja kuhusu Uislamu. Hakuna anayeweza kuuhodhi Uislamu. Hakuna anayeweza kuwa na amri juu ya ibada na kuwataabisha Waislamu kuifanya. Wenye kufanya hivyo, ikiwa wanaifanya kwa niaba ya Uislamu au ya Ujinga, wanamvunjia heshima Allah kwa sababu Allah anataka viondoshwe vikwazo vyote vyenye kuwazuia watu kumfikia. Zaidi ya hivyo, Amefaradhisha kufanya jihad dhidi ya vizuizi hivyo ili watu wajue, wajifundishe na waupokee Uislamu, ulio msafi na wenye kufahamika kirahisi, wenye kutangamana nao. Kuwanusuru watu dhidi ya utawala na uonevu wa watu wengine, dhidi ya mabwanyenye, wenye mamlaka, wahenga, mababa, mabwana na desturi wanazozing’ang’ania, na kuwawezesha kuufikia Uislamu, ambao ni mfumo na utukufu wa Allah, katika namna zote za maisha... Hivi ndivyo Uislamu ulivyo; mitume wote walitumwa kwa ajili ya hilo.
Kuupa Mamlaka Uislamu Maishani
Kanuni ambayo ni msingi mkuu wa Uislamu katika historia nzima ya mwanadamu ni ya “La ilaha illallah”. Yaani, kanuni ya kuuweka uungu, ubwana, utawala na mamlaka kwa Allah peke yake. Kanuni hii inapasa idhihirike kwa njia ya imani moyoni, ibada katika hisia, na vitendo na sheria na mfumo maishani. Kama mtu hashuhudii kuwa hakuna mwenye haki ya kuabudiwa isipokuwa Allah kwa njia inayofaa, huzingatiwa kuwa anamkosea heshima Allah na Uislamu.
Kanuni hii hutumika kikamilifu pindi mwanadamu anapomgeukia Allah kikamilifu katika maisha yake. Hivyo, mwanadamu anatazama hukumu za Allah katika mambo yote na hatua zote za maisha yake; anapokea na kutanguliza amri za Allah kuliko rai zake mwenyewe.
Mtu mwenye kutoa khabari na kuwafikishia watu hukumu za Allah ni Mjumbe wa Allah (s.a.w). Kanuni hii ndio inayounda sehemu ya pili ya kalima ash-shahada.
“Muhammad ni Mjumbe wa Mwenyezi Mungu.” (al-Fath, 48/29)
Hii ni sehemu ya pili ya kanuni ya msingi inayoegemewa na Uislamu. Kanuni hii itakapotekelezwa kikamilifu katika vipengele vyote vya kimaisha, mfumo kamili utaajitokeza. Huo ni mfumo anaouridhia Allah.
Lengo la Uislamu ni kuondoa Ujinga. Ni lazima kuweka wafanyakazi wapya tendaji wa kuweza kuutambua. Hili ni kundi la watu wanaofuata mbinu ya Kiislamu katika mtindo wao wa kimaisha, hali ya akili, mfumo wa kijamii, kiwango cha hukumu na njia, kwa kifupi, kila kitu. Ni hao tu ndio wanaoweza kuujenga tena umma wa Kiislamu na kustahiki kuwa ndio wanaotambulishwa na aya zifuatazo:
“Nyinyi mmekuwa bora ya umma walio tolewa watu, kwa kuwa mnaamrisha mema na mnakataza maovu, na mnamuamini Mwenyezi Mungu.” (Aal-i Imran, 3/110)
“Na vivyo hivyo tumekufanyeni muwe Umma wa wasitani, ili muwe mashahidi juu ya watu, na Mtume awe ni shahidi juu yenu...” (al-Baqara, 2/143)
Maswali juu ya Uislamu